• ePaper
Thursday, April 23, 2026
  • Login
No Result
View All Result
Uhuru Publication
  • Habari
  • Michezo
  • Uchaguzi
  • Burudani
  • Toleo Maalumu
  • Kolamu
  • Makala
  • Hadithi
  • Habari
  • Michezo
  • Uchaguzi
  • Burudani
  • Toleo Maalumu
  • Kolamu
  • Makala
  • Hadithi
  • Login
No Result
View All Result
ePaper
Uhuru Publication
Home Habari

IJUE SHERIA MPYA YA FIDIA KWA ABIRIA WA NDEGE 

Abdurahman Jumanne by Abdurahman Jumanne
December 21, 2025
in Habari, Kitaifa, Makala
0
IJUE SHERIA MPYA YA FIDIA KWA ABIRIA WA NDEGE 
0
SHARES
14
VIEWS
Share on FacebookShare on Twitter

Na Adv. Ramadhani A. Maleta

  1.   UTANGULIZI

Katika kuhakikisha haki za abiria wanaotumia usafiri wa anga zinalindwa na viwango vya fidia vinaboreshwa, Serikali  kupitia Wizara ya Uchukuzi, hivi karibuni imetunga kanuni au sheria ndogo mpya ya kusimamia  taratibu za kisheria za kushughulikia madai ya fidia kwa wahanga wa usafiri wa anga hususan pale inapotokea ajali ya ndege inayosababisha  vifo au majeraha ya kimwili kwa abiria.

Kanuni hizi kimsingi ndiyo sheria inayopaswa kutumika hapa nchini  katika kushughulikia kesi za madai au migogoro yote inayotokana na  safari za  ndege zinazofanyika ndani ya mipaka ya Tanzania, ambazo kitaalam zinajulikana kama domestic flights Operations.

Madai au migogoro inayosimamiawa na kanuni au sheria hiyo mpya ni pamoja na yale yanayohusiana na malipo ya fidia kutokana na vifo au majeraha kwa abiria yanayosababishwa na ajali za ndege.

Pia kanuni au sheria hii pia inashughulikia madai ya fidia kwa abiria wanapopata madhara mengine ya kibiashara, kiuchumi na kisaikolojia wakiwa safarini, ikiwemo kupotelewa au kuharibikiwa na mizigo, kuachwa na ndege, abiria kucheleweshwa au kufutwa kwa safari za ndege walizopangiwa na wakati mwingine abiria kukataliwa kusafiri katika ndege aliyopangiwa wakati ana tiketi halali.

Makala hii inaelezea kwa ufupi baadhi ya mambo muhimu yaliyomo katika sheria hiyo mpya ya mwaka 2024.

2.0 KANUNI MPYA ZA FIDIA ZA MWAKA 2024

Kama nilivyogusia katika utangulizi hapo juu, kuanzia mwaka 2024, Tanzania imepata kanuni au sheria ndogo mpya za kusimamia madai  na viwango vya  malipo ya fidia kwa abiria wanaotumia usafiri wa anga pindi inapotokea ajali ya ndege na kusababisha vifo au majeraha kwa abiria husika.    

Kanuni au Sheria hiyo pia inajumuisha haki ya fidia kwa abiria wanaopata madhara mengine, ikiwemo kupata hasara za kibiashara, kiuchumi na kisaikolojia wanapokuwa wanatumia usafiri wa anga kama zilivyoainishwa kwenye utangulizi.

Kanuni au sheria hiyo mpya inajulikana kwa kiingereza kama The Civil Aviation (Carriage by Air) Regulations ya mwaka 2024, ambayo ipo kupitia Tangazo la Serikali (G.N. Na 4 la Mwaka 2024). Sheria hii ndogo  ijulikanayo kitaalamu kama Subsidiary Legislation, imetungwa na Waziri  wa Uchukuzi ambaye ndiye mwenye dhamana ya masuala ya Usafiri wa Anga hapa nchini, kwa mamlaka aliyopewa na kifungu cha 4 cha Sheria ya Usafiri wa Anga ijulikanayo kama The Civil Aviation Act, (Cap 80, R.E. 2024 ).

Ifahamike pia kwamba, kanuni au sheria hii mpya ya mwaka 2024  inaifuta na kuchukua nafasi ya  kanuni au sheria iliyokuwepo awali  ambayo ilijulikana kama The  Civil Aviation (Carriage by Air) Regulations, ya mwaka 2008  ambayo pia ilikuwa sheria ndogo iliyotungwa na Waziri wa Uchukuzi.

Pia ifahamike kwamba kanuni au sheria hii mpya ya mwaka 2024 kama ilivyokuwa kwa kanuni au sheria iliyopita ya mwaka 2008, inatumika  hapa nchini kwa kusimamia madai ya fidia yanayotokana na safari za ndege zinazofanya shughuli zake ndani ya mipaka ya Tanzania (domestic flights), kwa mfano ndege zinazotoka mkoa mmoja kwenda mkoa mwingine pasipo kutoka nje ya mipaka ya nchi.

Hii maana yake ni kwamba, kwa madai ya fidia yanayohusiana na ndege zinazofanya safari za kimataifa (international flights) kwa kuvuka mipaka ya Tanzania, kanuni au sheria hii ya mwaka 2024 haitumiki pindi  madai au migogoro  ya fidia kwa abiria wanaotumia ndege kama hizo za kimataifa  yanapojitokeza. Badala yake, kuna sheria nyingine tofauti inayotumika kushughulikia madai yanayotokana na ndege kama hizo  zinazofanya safari za kimataifa ijulikanayo kama Mkataba wa Kimataifa wa Montreal wa mwaka 1999, maarufu kama The Montreal Convention of 1999.

Ifahamike kwamba, mkataba huu wa mwaka 1999 ndiyo sheria ya kimataifa ambayo  inampa haki raia wa nchi yoyote wakiwemo Watanzania kudai fidia dhidi ya shirikika la ndege la nchi yoyote linapopata ajali popote duniani wakati likifanya safari za kimataifa na  mtu huyo kupata ajali inayopelekea kifo au majeraha akiwa ni mmoja wa abiria katika ndege husika. 

Kwa bahati nzuri, ili kumrahisishia abiria kama huyo kuepukana na  gharama na mambo mengine yanayoweza kumfanya ashindwe kumudu kuendesha kesi kama hiyo katika mahakama za nchi za nje, Mkataba huo wa mwaka 1999 kama sheria ya kimataifa, unampa haki abiria kama huyo chini ya kifungu cha 33 kufungua kesi dhidi ya shirika la ndege husika katika  mahakama ya nchi ambayo abiria husika  amekuwa akiishi, pasipo kujali uraia wa abiria huyo.  Pia haijalishi kama  ni wapi ajali husika ilitokea na shirika la ndege husika ni la nchi gani.    

3.0   KIWANGO CHA FIDIA KWA VIFO NA MAJERAHA

Kwa mujibu wa kifungu cha aircraft cha 18(1) cha Kanuni au Sheria hii mpya ya mwaka 2024, abiria atastahili kulipwa fidia pale mambo yafuatayo yatakapothibitika: (i) kwamba ajali husika ya ndege imetokea, (ii) kwamba ajali hiyo imesababisha vifo au majeraha kwa abiria; na (iii) kwamba abiria husika walikufa au kupata majeraha ya kimwili (bodily injuries) wakiwa ndani ya ndege husika (on board the aircraft) au wakiwa katika mchakato wa kupanda au kushuka katika ndege husika (in the process of embarking or disembarking). Pindi mambo hayo matatu  yatakapothibitika, mwenye ndege hatakuwa na chaguo au utetezi wowote zaidi ya kuwajibika (strictly liable) chini ya kifungu cha 29 (1) kulipa fidia inayofikia fedha za kitanzania sawa na Special Drawing Rights (SDR) 100,000 kwa kila abiria aliyekufa au kujeruhiwa katika ajali hiyo. SDR ni fedha ya kimataifa ambayo thamani na kiwango chake kinapangwa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) SDR kama hizo 100,000 zinafikia Dola za Kimarekani 120,000. 

Hii maana yake ni kwamba kiwango cha fidia tajwa hapo juu kitalazimika kulipwa na mwenye ndege inapothibitika tu kwamba ajali ya ndege imetokea na kusababisha vifo au majeraha kwa abiria. Hii haijalishi kama ajali husika ilisababishwa na makosa au uzembe wa wenye ndege au hapana, kwani kigezo pekee kinachomwajibisha mwenye ndege kulipa fidia hiyo ya SDR 100,000 kila abiria  ni uthibitisho wa uwepo wa ajali ya ndege na vifo au majeraha kwa abiria.  

Hata hivyo, kwa mujibu wa kifungu cha 29(2) kama abiria au ndugu wa marehemu hawataridhika na kiwango hicho kilichowekewa ukomo (limited claim) cha fidia ya SDR 100,000 na wakaamua kudai malipo zaidi ya hayo, sheria hiyo inatoa haki kwa watu kama hao kuwasilisha mahakamani madai ya kuomba malipo ya fidia ya ziada kwa kiwango chochote (unlimited claim) kadri wanavyoona inafaa. Hata hivyo, ili mtu kama huyo aweze kufanikiwa kulipwa malipo kama hayo ya fidia ya  ziada, atalazimika kuithibitishia mahakama kwamba ajali husika ilisababishwa na ama kutowajibika (omission) au uzembe (negligence) wa ama mwenye ndege, watumishi wake au mawakala wake.

Kwa upande mwingine, mwenye ndege naye ana haki ya kujitetea  katika hatua hii kwa kupinga kulipa malipo kama hayo ya fidia ya zaidi ya SDR 100,000 kwa kuithibitishia mahakama kwamba yeye kama mmiliki wa ndege husika pamoja na watumishi au mawakala wake, waliwajibika ipasavyo kuhakikisha usalama wa ndege na abiria wake na hawakuhusika na uzembe wa aina yoyote uliopelekea kutokea kwa ajali na vifo au majeraha husika. Hii ni kwa mujibu wa kifungu cha 29(2)(a) cha kanuni au sheria hiyo ya waka 2024.

Mbali  na utetezi kama huo, mwenye ndege anaweza pia chini ya kifungu cha 29(2)(b),  kukwepa adhabu  kama hiyo ya kutakiwa kulipa  fidia ya ziada, kama ataithibitishia mahakama kwamba, ajali husika ilisababishwa na mtu mwingine (a third part) ambaye hana mahusiano naye na hakuwa na uwezo wa kumdhibiti. Kwa mfano ajali inaposababishwa na shambulio la kigaidi.

Lakini pia mwenye ndege atajiokoa katika kutakiwa kulipa malipo kama hayo ya fidia ya ziada, kama atajitetea kwa kuithibitishia mahakama kwamba kifo au majerha ya abiria husika vilichangiwa na uzembe wa abiria mwenyewe (contributory negligence). Kwa mfano, kama wahudumu wa ndege walitoa ilani ya hatari na kuwataka abiria wote kutulia katika viti vyao na kufunga mikanda, lakini abiria husika alikaidi maelekezo hayo kwa kutofunga mkanda na hatimaye kupata madhara, hawezi kulipwa fidia kama hiyo ya ziada, kwa vile kisheria anachukuliwa kuwa alifanya uzembe uliochangia madhara yaliyompata.

Wiki ijayo tutaendelea kuangalia sheria hiyo mpya katika vipengele vya fidia kwa upotevu na uharibufu wa mizigo ya abiria pamoja na abiria kucheleweshwa safari au kufutwa kwa safari za ndege.  

Previous Post

WAZIRI MKUU: WIZARA YA AFYA FUATILIENI UPATIKANAJI WA DAWA MAHSUSI

Next Post

MADAKTARI BINGWA WAFUNGUKA MBINU KUKABILI ‘PRESHA’

Next Post
MADAKTARI BINGWA WAFUNGUKA MBINU KUKABILI ‘PRESHA’

MADAKTARI BINGWA WAFUNGUKA MBINU KUKABILI ‘PRESHA’

Leave a Reply Cancel reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Recommended

WASIRA : VIJANA MSIKUBALI KUTUMIKA KUVURUGA AMANI

WASIRA : VIJANA MSIKUBALI KUTUMIKA KUVURUGA AMANI

5 months ago
MIKOPO YA SERIKALI KWA VIJANA, FURSA MPYA KUKUZA UCHUMI WA UVUVI

MIKOPO YA SERIKALI KWA VIJANA, FURSA MPYA KUKUZA UCHUMI WA UVUVI

1 month ago

Popular News

  • NDEJEMBI ATAJA VIPAUMBELE 10 SEKTA YA NISHATI

    NDEJEMBI ATAJA VIPAUMBELE 10 SEKTA YA NISHATI

    0 shares
    Share 0 Tweet 0
  • MWIGULU ATOA MAAGIZO ALAT

    0 shares
    Share 0 Tweet 0
  • RIPOTI YA KUPONYA

    0 shares
    Share 0 Tweet 0
  • MWANDAAJI MISS WORLDTZ AITAJA AMANI

    0 shares
    Share 0 Tweet 0
  • SIMBA, MAFUNZO HAPATOSHI

    0 shares
    Share 0 Tweet 0

Stay Update, Subscribe Now!

Check your inbox or spam folder to confirm your subscription.

Ukurasa Rasmi wa Televisheni ya Gazeti la Uhuru.

Facebook-f Instagram X-twitter Youtube tiktok
Quick Links
  • Habari
  • Michezo
  • Uchaguzi
  • Burudani
  • Toleo Maalum
  • Kolamu
  • Makala
Services
  • ePaper
Contact Information
  • Dar es Salaam,Tanzania
  • info@upl.co.tz
  • +255 783 925 742
Uhuru Publications , 2025 © All Rights Reserved
  • Terms & Conditions
  • Privacy Policy
  • FAQ
No Result
View All Result
  • Home
  • Habari
  • Michezo
  • Uchaguzi
  • Burudani
  • Toleo Maalumu
  • Kolamu
  • Makala
  • Contact
  • Hadithi

© 2026 JNews - Premium WordPress news & magazine theme by Jegtheme.

Are you sure want to unlock this post?
Unlock left : 0
Are you sure want to cancel subscription?