Na ELIZABETH JOHN
MADAKTARI bingwa wa magonjwa ya moyo wameeleza njia mbalimbali za kukabiliana na tatizo la shinikizo la damu ‘presha’, ambalo linasumbua wananchi wengi kutokana na mabadiliko ya mtindo wa maisha na changamoto za kiafya.
Hatua hiyo, imekuja baada ya tatizo hilo kuwakumba watu wengi wakiwemo ambao huko nyuma hawakuwa wakisumbuliwa nalo hususan watu wa kipato cha chini, watoto na vijana.
Akizungumza na UHURU jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dk. Delilah Kimambo, alisema msingi wa kukabiliana na presha unaanzia katika lishe bora.
Alisema wananchi wanapaswa kupunguza matumizi ya chumvi na vyakula vyenye mafuta mengi yasiyo ya asili, huku wakiepuka vyakula vya kusindika kama soseji na vyakula vya mikononi, badala yake waongeze kula matunda na mboga za majani.
“Pia kudhibiti uzito wa mwili ni hatua muhimu, kwani uzito uliopitiliza huongeza mzigo kwa moyo na kusababisha presha kupanda. Kufanya mazoezi ya mwili mara kwa mara ni silaha muhimu dhidi ya presha, hasa kwa watu wanaoishi maisha ya kukaa muda mrefu bila harakati.
“Zamani watu walikuwa wanatembea umbali mrefu kufuata mahitaji yao ya kila siku, lakini kwa sasa hata safari fupi watu hutumia vyombo vya usafiri kama bodaboda, hali inayopunguza sana mazoezi ya mwili.
“Pia shughuli za kilimo na kazi za mikono zilikuwa sehemu ya maisha ya kila siku kwa watu wengi, lakini sasa vijana wengi hawajihusishi na kazi hizo,” alisema.
Alisema msongo wa mawazo nao ni adui mkubwa wa afya ya moyo, hivyo inashauriwa watu kujifunza njia za kupunguza mawazo, ikiwemo kupumzika, kupanga ratiba nzuri za kazi na kushiriki shughuli za burudani.
Aidha, Dk. Delilah alionya matumizi ya pombe kupita kiasi na sigara, tabia hizo huathiri mishipa ya damu na kuongeza hatari ya shinikizo la damu.
Mkurugenzi huyo alisema upande wa umri na sababu za kurithi, ingawa haviwezi kuepukika, mtu anaweza kupunguza athari zake kwa kuzingatia mtindo bora wa maisha na kupima presha mara kwa mara.
Kwa upande wake, Dk. Ahmed Ibrahimu kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), alisema wagonjwa wenye magonjwa mengine kama kisukari, figo au matatizo ya tezi wanapaswa kuwa makini zaidi, kwa kuwa magonjwa hayo yanaweza kuchochea presha.
Pia, alitoa tahadhari kuhusu matumizi ya baadhi ya dawa, zikiwemo za kuzuia mimba, dawa za kupunguza msongo wa mawazo na dawa za pumu, akisisitiza umuhimu wa kupata ushauri wa kitaalamu kabla ya kuzitumia kwa muda mrefu.
Daktari huyo alisisitiza kwamba kukabiliana na presha kunahitaji mabadiliko ya mtindo wa maisha, uelewa wa afya binafsi na ushirikiano wa karibu na wataalamu wa afya ili kulinda maisha na kuimarisha afya ya jamii kwa ujumla.
Dk. Tulizo Shemu kutoka JKCI, alisema mabadiliko ya hali ya maisha ndiyo sababu kubwa ya ongezeko la idadi kubwa ya wagonjwa wa shinikizo la damu.
“Ni hatari zaidi kula chumvi nyingi hasa mbichi, mafuta na vitu vya kusindikwa, ukitaka kuwa na afya nzuri kula sana mboga za majani na matunda na mazoezi kidogo, huu ugonjwa utakuwa umeukimbia,” alisema.
Alisisitiza kuwa kufanya mazoezi ya mara kwa mara, hata matembezi ya kawaida, ni njia muhimu ya kupunguza ongezeko la wagonjwa wa shinikizo la damu na kuboresha afya kwa ujumla, akihimiza jamii kubadili mtazamo na kuchukua hatua mapema.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), hadi Machi mwaka huu, watu milioni 1.13 wamegundulika kuwa na shinikizo la damu duniani.
Mei 17 ya kila mwaka huadhimishwa siku ya shinikizo la damu duniani, siku maalumu ya kueneza ufahamu kuhusu tatizo hilo.




