Na ZIANA BAKARI
WATU wenye umri zaidi ya miaka 40 na uzito kupindukia, wapo hatarini kupata presha ya macho, iwapo hawatozingatia namna sahihi ya kuyatunza, imeelezwa.
Hivyo, wametahadharishwa hali hiyo itawasababishia kushindwa kuona kabisa, endapo hawatapata matibabu kwa wakati.
Hayo yalibainishwa Dar es Salaam na Daktari wa macho wa Kituo cha Msimbazi, Zacharia Mitarambo, alipozungumza na UHURU kuhusu umuhimu wa kuchukua hatua kuepuka matatizo ya macho.
Dk. Mitarambo aliwataja watu wengine waliopo hatarini kupata presha ya macho ni wenye historia ya ugonjwa wa macho katika familia zao, wanaotumia dawa za ‘steroids’ kwa muda mrefu, ambazo zinaweza kupunguza kinga mwilini.
“Kadri umri unavyoongezeka miundo ya ndani ya jicho hupungua ufanisi wake wa kutoa maji na kuongeza shinikizo ndani ya jicho. Siku zote presha ya macho inatakiwa kuwa 10 hadi 21 na haitakiwi kuzidi hapo.
“Tunapaswa kujua ndani ya jicho kuna aina mbili za uoni, ambazo ni uoni wa pembeni na uoni wa kati,” alisema.
Dk. Mitarambo alibainisha uoni wa pembeni ni wa kwanza kuharibika, kabla ya wa kati, hivyo wananchi wanapaswa kupima macho, kila mwaka kubaini matatizo mapema na kuyatibu. Aliwashauri wananchi kupima presha ya macho.
Akizungumzia presha ya macho, mtaalamu huyo alieleza ni hali ya kuharibika uoni wa kuona, unaounganisha jicho na ubongo, kutokana na presha kubwa ndani ya jicho.
Alisema tatizo la uoni wa pembeni kuharibika, husababishwa na presha ya macho kuzidi kuongezeka sehemu kubwa ya jicho hadi kutoona vizuri.
Mtaalamu huyo alibainisha iwapo katika familia kuna historia ya matatizo ya macho, upo uwezekano mkubwa wa kupata presha ya macho kwa sababu baadhi hurithiwa.
Kwa mujibu wa mtaalamu huyo, presha ya macho hutokea pale kiwango cha uzalishaji maji ndani ya jicho kushindwa kutoka nje ya mfumo, hivyo kuziba kwa mirija inayopitisha kutengeneza usawa wa kiwango kinachotakiwa.
Dk. Mitarambo alisema presha ya macho inapozidi kiwango husababisha mshipa wa fahamu kuharibika na kupoteza nguvu ya kuona na kiwango cha nguvu ya kuona kilichokufa hakirekebishwi kwa njia yoyote.
“Kiwango hicho kitakapokufa, itamlazimu mtu atumie dawa za kupunguza presha ya macho kwa maisha yake yote au kufanyiwa upasuaji kutengeneza mirija mbadala ya kutolea maji, njia ambayo siyo bora.
“Ninawasihi wananchi hususan wenye matatizo ya presha ya macho, kuzingatia matumizi sahihi ya dawa na kuhakikisha familia zao zinahudhuria kliniki ya macho kupima tatizo hilo,” alieleza mtaalamu huyo.
Mkazi wa Ilala, Dar es Salaam, Maria John, aliwasihi wananchi kuweka utaratibu wa kupima macho mapema, kuepuka kupata madhara makubwa baadaye.
“Ninawasihi wananchi wenzangu, tujitahidi tunapopima magonjwa mengine hospitalini, tusisahau kupima macho. Kupima mapema kunakusaidia kupata matibabu kwa wakati na kuepuka madhara makubwa yanayoweza kutokea baadaye,” alisema.




