Na AMINA KASHEBA
RAIS Dk.Samia Suluhu Hassan ametoa maagizo kwa Kocha wa Taifa ‘Taifa Stars’Miguel Gamondi kama kuna kijana Mtanzania ana kipaji na anafanya vizuri kule alipo, amuite kuja kuchezea timu hiyo.
Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, alipozungumza maelekezo aliyopewa na Rais Dk. Samia, baada ya tukio la kutia saini mkataba wa kocha huyo.
“Maelekezo ya Rais Dk.Samia Suluhu Hassan amesema kuwa mwambie Gamondi kama kuna kijana wa Kitanzania kokote duniani amlete hapa katika taifa lake kwa lengo la kujiunga na kikosi, ili timu ifanye vizuri na kombe la AFCON 2027 libaki nchini.
“Kocha Gamondi amepewa uwanja mpana zaidi pale anapoona kijana yupo Hispania, Uarabuni, Marekani ama nchi yoyote, lakini ni Mtanzania ana kipaji na anafanya vizuri kule alipo, Rais ametupa kibali cha kuwaita wote kuja kuchezea timu yao ya taifa,”amesema.
Katika hafla hiyo, Makonda alifuatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa pamoja na Rais wa Shirikisho la Miguu wa Miguu Tanzanía (TFF) Walace Karia alisema kocha huyo anatakiwa kuanza kuandaa programu za kuwanoa wachezaji kuelekea mashindano ya AFCON 2027.
Waziri huyo alifafanua kwamba Gamondi alifanya vizuri katika mashindano ya AFCON yaliyofanyika nchini Morocco na timu kumaliza hatua ya 16 na kuonesha kiwango kikubwa, ndiyo maana wamempatia fursa ya kukinoa kikosi cha Stars kuelekea AFCON 2027.
“Wote tumeshuhudia Gamondi alipewa timu ndani ya muda mchache, lakini mabadiliko yalionekana na wachezaji walifika hatua ya 16 na kuacha historia kubwa pale nchini Morocco, hivyo serikali imeona ipo haja ya kumpatia mkataba wa kuinoa Stars atahudumu ndani ya miaka miwili.
“Gamondi anapaswa kufahamu serikali imewekeza fedha kwake, hivyo anatakiwa kukinoa vyema kikosi ili kifanye vizuri na kubakisha kombe nyumbani, pia kupanda viwango sio CAF hadi FIFA,” alisema.
Makonda alisema lengo la kufanya hivyo ni kuwapa furaha Watanzania wote na kusisitiza haiwezekani mashindano ya AFCON 2027 yaandaliwe nchini halafu Tanzania iwe ya kwanza kutoka.
Waziri huyo alisema fedha za malipo za mishahara ya kocha huyo, zitalipwa na serikali chini ya Rais Dk. Samia hivyo anahitaji kikosi hicho kinolewe vizuri na kufanya vizuri katika mashindano yanayokuja.
Rais wa TFF, Walace Karia alishukuru serikali kwa uwekezaji mzuri wa miundombinu na sapoti kubwa katika michezo hasa mpira wa miguu.
“Tunashukuru serikali kwa sapoti kubwa katika michezo hasa soka, kama shirikisho tutafanya kazi kwa bidii na kufanya mchezo huu kuwapa watu furaha na kupeperusha vyema bendera ya taifa,” alisema.
Kocha, Gamondi alisema anajisikia fahari kuwa kocha mkuu wa timu hiyo na kuahidi kushirikiana na taasisi mbalimbali kuhakikisha Stars inapanda viwango katika mpira wa miguu duniani.
“Nashukuru kwa kuwa kocha mkuu wa Stars, nimefurahi naipenda Tanzania nitahakikisha nashirikiana vizuri na taasisi za soka nchini ili timu ifanye vizuri na kuonesha soka bora na kupanda viwango Afrika na duniani nzima,” alisema kocha huyo.
Wakati huo huo, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amelitaka Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kufanya kikao na vyama vya michezo mbalimbali kujadili namna ya kufanya vizuri kimataifa.
Akizungumza Dar es Salaam, Waziri huyo alisema wanahitaji kuona vyama na mashirikisho hayo ya michezo mingine kuhakikisha yanafanya vizuri kama ilivyo TFF.
Alisema Tanzania kuna michezo mingi ambayo inapaswa kufanya vizuri na kupeperusha bendera ya taifa katika mashindano ya kimataifa.
“Natoa maagizo kwa BMT kukaa na kufanya kikao na vyama na mashirikisho ya michezo kujadili namna gani wanaweza kufanya vizuri katika ngazi ya kimataifa.
“Tunahitaji kushinda medali na makombe kwani kuna michezo mingi ambayo inapaswa kufanya vizuri na kuwapa furaha Watanzania,” alisema.
Waziri huyo alisema kuna vijana wengi mtaani wana vipaji hivyo viongozi wa vyama na mashirikisho wanatakiwa kuliangalia jambo hilo.
“Kama kuna kiongozi wa chama au shirikisho ambaye anagombea uongozi kila wakati ukifika halafu mchezo huo haufanyi vizuri, mnatakiwa kutompa fomu ya kugombea maana haleti faida,” alisema.




