Na MWANDISHI MAALUMU, Arusha
MAKAMU wa Rais, Dk. Emmanuel Nchimbi, ameihakikishia Jumuiya ya Nchi za Afrika, Karibiani na Pasifiki (OACPS), dhamira ya Tanzania kuendelea kutoa ushirikiano kwa taasisi hiyo katika kuleta mageuzi na kuifanya kuwa na tija kwa nchi wanachama.
Dk. Nchimbi alisema hayo jijini Arusha, alipokutana na Katibu Mkuu wa OACPS, Moussa Batraki.
Alimpongeza katibu huyo kwa kutekeleza ajenda ya mageuzi ikiwemo kuongeza uadilifu na kupunguza utegemezi kwa lengo la kufanya taasisi hiyo kuwa na nguvu zaidi.
Kwa upande wake, Batraki alieleza vipaumbele vya taasisi hiyo ikiwemo suala la kuimarisha biashara, mtangamano miongoni mwa nchi wanachama sanjari na kujenga uhimilivu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Pia, alieleza dhamira ya taasisi hiyo ya kuweka kipaumbele na uwekezaji katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), hususan katika teknolojia za kidijitali, Akili Unde (AI), ulinzi na usimamizi wa takwimu na taarifa.
Aidha, kuimarisha uhusiano wa kibiashara miongoni mwa nchi zinazoendelea na kuwajengea uwezo wanawake katika masuala ya kiuchumi.
Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji na Umoja wa Ulaya, Jestas Nyamanga na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Ellen Maduhu.



