Pwani
Na Mwamvua Mwinyi
MKUU wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge, amesema uzinduzi wa mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), utakaofanyika kesho wilayani Rufiji mkoani hapa, ni atua kubwa ya kihistoria katika kuimarisha upatikanaji nishati ya uhakika nchini.
Mradi huo wenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 za umeme unaotekelezwa kwa asilimia 60 katika Mkoa wa Pwani na asilimia 40 katika Mkoa wa Morogoro, unaonyesha dhamira ya serikali kuhakikisha Tanzania inakuwa na umeme wa kutosha kwa ajili ya kuchochea shughuli za uzalishaji.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kunenge alisema mkoa wa Pwani unajivunia kuwa mwenyeji wa mradi huo mkubwa wa kimkakati.
“Mradi huu ulianza kutekelezwa kuanzia Serikali ya Awamu ya Tano. Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aliupokea ukiwa umefikia asilimia 30 ya utekelezaji, lakini sasa ameukamilisha hatua aliyofanikisha kutimizwa ndoto ya mwasisi wa mradi huo, Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Alisisitiza: “JNHPP ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati ya nishati nchini, ukitarajiwa kusafirisha umeme kupitia njia mbalimbali za Gridi ya Taifa na vituo vya kupozea umeme vya Chalinze–Kinyerezi, Kwala–Zegereni–Zinga na Dundani–Msufini Mkuranga.”
Katika hatua nyingine, Kunenge alisema sekta ya viwanda na uwekezaji imeendelea kukua kwa kasi mkoani Pwani, ambapo kuna jumla ya viwanda vikubwa na vya kati 495.
Kuhusu uhifadhi wa vyanzo vya maji, Kunenge aliwataka wananchi kutunza vyanzo hivyo na kulinda mazingira yanayozunguka bwawa hilo.
Sanjari na matumizi ya maji kwa ajili ya uzalishaji wa umeme, alibainisha kwamba serikali inapanga kujenga bwawa la maji safi litakalotumika kwa matumizi ya wananchi wa Pwani na Morogoro, huku mpango huo ukitarajiwa kunufaisha hadi Mkoa wa Lindi.




