Na NJUMAI NGOTA, Mwanza
MGOMBEA Mwenza wa Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, ametaja baadhi ya mambo muhimu ambayo wamedhamiria kuyatekeleza katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Miongoni mwa mambo hayo ni kuimarisha miundombinu, sekta ya elimu, afya na nishati.
Pia, mfumo wa ufuatiliaji miradi ya maendeleo utaboreshwa zaidi kwa kuziba mianya ya ucheleweshaji na ubadhirifu, itekelezwe kwa ubora na ufanisi.
Balozi Dk. Nchimbi, alisema hayo akiwa Kata ya Mwankulwe, wilayani Kwimba, mkoani Mwanza, alipowahutubia mamia ya wananchi, waliohudhuria uzinduzi wa kampeni za CCM.
Kupitia mkutano huo, Dk. Nchimbi, alimwombea kura mgombea urais, Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Kwa Wilaya ya Kwimba, Chama kimedhamiria kuboresha na kuimarisha zaidi huduma za afya, kujenga zahanati mpya 20.
“Ukiamka tu unaumwa, ukitoka nje unaiunua macho yako, unatazama, eneo siyo mbali kuna zahanati, hicho ndicho ambacho tungependa kiwe.
“Siyo unatembea kwenda zahanati wakati unatoka nyumbani kwako unaumwa kichwa, ukifika zahanati unaumwa miguu… hicho ndicho tulichodhamiria kukifanya katika kipindi cha miaka mitano ijayo,” alisema.
SEKTA YA AFYA
Balozi Dk. Nchimbi, alitaja jambo la pili ambalo wamekusudi kulifanya ni kukamilisha ujenzi wa zahanati nne, ambazo zipo hatua mbalimbali ambapo katika kipindi cha miaka mitano, zitakamilika haraka, ziwe mpya 24 na hizo 20.
Kwa mujibu wa Dk. Nchimbi, katika kipindi hicho, wanatarajia kujenga vituo vipya vya afya Kwimba.
“Mnajua kituo cha afya uzito wake, vinakaribiana na zahanati, vituo vya afya vinaweza kulaza wagonjwa, vinaweza kutibu magonjwa ambayo yameshindikana katika zahanati, ukitoka zahanati uende hatua ya juu, hivyo tumekusudia kuwa na vituo vipya vya afya vitano,”alisema.
Mgombea mwenza huyo, alisema katika hospitali ya wilaya, wamekusudia kuimarisha huduma za kibingwa, huduma za magonjwa sugu, magonjwa yanayotakiwa kwenda hospitali kubwa zaidi, zipatikane katika hospitali hizo.
ATOA MSISITIZO
Balozi Dk. Nchimbi, alisisitiza kauli ya Mgombea Urais wa CCM, Dk. Samia, aliyoitoa juzi katika uzinduzi wa kampeni zilizofanyika viwanja vya Tanganyika Parkers, Dar es Salaam, kuhusu Bima kwa Watanzania Wote, ambayo watawapa wajawazito, watoto na wenye ulemavu katika kipindi cha siku 10.
Alisema Watanzania hao, watapatiwa huduma hiyo siku 100 za kwanza, kwani kundi hilo linaumiza zaidi kutokana na changamoto ya afya.
Dk. Nchimbi alisema wamedhamiria kuimarisha zaidi miundombinu sekta ya elimu kwa kuongeza madarasa, walimu na kuboresha mitaa.
“ Tunataka watoto wetu wasikae tu madarasani, waweze kufundishwa, kuelimika na kufaulu,”alisema.
Pia, Balozi Dk. Nchimbi, alitaka kila mtoto aende shule, hivyo katika miaka mitatu ya kwanza, wamedhamiria wanafunzi wa darasa la kwanza hadi la tatu, wafahamu kusoma, kuandika na kuhesabu bila shida yoyote.
Alisema katika kipindi cha miaka mitano, wananchi wa Kwimba 90 kati yao 100 wapate maji safi na salama.
Alisema watahakikisha mbolea, pembejeo, mbegu na dawa, zinapatikana kwa bei nafuu na kwa wakati.
Balozi Dk. Nchimbi alisema wamedhamiria kuimarisha masoko ya bidhaa za mashambani , wakulima waone tija ya kilimo wanachokifanya.
Mgombea Mwenza huyo wa Urais alisema wamedhamiria kuongeza viwango vya barabara za lami kufikia kilometa 120.
Pia, Balozi Dk. Nchimbi alisema wataboresha barabara za changarawe.
Alisema wataboresha na kuimarisha huduma za nishati kwa kuhakikisha kila mwananchi na kijiji wanapata huduma hiyo.
Alisema katika kipindi cha miaka mitano wamedhamiria kurasimisha biashara ambazo hazijarasimishwa kwa kuboresha biashara za bodaboda, kuongeza, kujenga na kuimarisha zaidi mitaji midogo kwa wafanyabiashara.
MAFANIKIO ILANI YA CCM 2020-2025
Balozi Nchimbi, alieleza kuwa, baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika miaka minne ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, Kwimba wameongezewa vituo vya afya kutoka 50 hadi 61, ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kwimba, shule za sekondari kutoka 34 hadi 43 na vijiji vilivyo na umeme kutoka 60 hadi 119.
Pia, shule za msingi zimeongezeka kutoka 154 hadi 161, watumishi wa afya kutoka 335 hadi 513, madarasa 56 hadi 77, maji safi safi asilimia 56 hadi 77.
Balozi Dk. Nchimbi alisema kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatika katika kipindi hicho, hivyo wataongeza kasi ya ujenzi wa zahanati mpya 20, vituo vya afya vitano na kuhakikisha huduma za kibingwa zinapatikana katika hospitali ya wilaya.
Pia aliahidi miradi ya maji kufikia asilimia 90 ya upatikanaji, pembejeo nafuu kwa wakulima na barabara za lami kilometa 120 ndani ya miaka mitano.
Dk. Mchimbi aliwaomba wana Kwimba kumpigia kura za kishindo Dk. Samia kwa kuwa, amefanya kazi kubwa kuleta maendeleo mkoani Mwanza na taifa kwa ujumla.




