Na HANIFA RAMADHANI,
Zanzibar
MGOMBEA Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewataka wananchi wapenda amani, kuiunga mkono CCM, ishinde kwa kishindo Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, mwaka huu.
Dk. Mwinyi, aliyasema hayo, katika mkutano wa hadhara wa Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, katika Kijiji cha Kajengwa, Jimbo la Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.
Alisema hamasa ya kujitokeza kwa wingi katika mikutano ya kampeni, ni jambo moja, lakini Uchaguzi ni siku ya kupiga kura, hivyo Oktoba 29, watu wajitokeze kwa wingi kushiriki tukio hilo la kuwachagua viongozi wanaotokana na CCM.
Alisema wakifanya hivyo, itakuwa vyema kama ulivyokuwa mwitikio wa watu wakati wa uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.
“Hakikisheni wote waliojiandikisha wanajitokeza kwa wingi, siku ikifika waende wakapige kura mapema, tupate ushindi wa kishindo,” alisisitiza.
Dk. Mwinyi ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, aliendelea kuhimiza muhimu wa kudumisha amani, umoja na maridhiano nchini, kwa sababu ndiyo sera namba moja ndani ya Ilani ya Chama.
Alisema wote wanatambua bila ya amani, umoja, mshikamano na maridhiano, hakuna jambo lolote linaloweza kufanyika, likawezekana.
Alisema wakimsikia mtu anasema kinyume, watambue huyo hawatakii mema, jambo la msingi ni kuendelea kuiunga mkono CCM, ndicho Chama kinachohubiri amani nchini.
Akizungumzia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi kwa Zanzibar na Tanzania bara, Dk. Mwinyi alisema wameitekeleza kwa kiwango kikubwa katika sekta zote.
“Tumeahidi na tumetekeleza na kulisema moja moja, itachukua muda mwingi, lakini ninyi wananchi hamhitaji kuelezwa, kwani yanaonekana wazi, ukitoka mjini kuja huku, mtayaona mengi sana tuliyoyatekeleza,” alisema
Alisema hana shaka kwamba, wote wanaridhika na utekelezaji wao kwa Tanzania bara na Zanzibar, kwa sababu mambo makubwa yamefanyika na mengine zaidi yatafuata.
Mgombea huyo, alimwombea kura Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan na kujiombea kura mwenyewe pamoja na wagombea wote wa ubunge Tanzania bara na visiwani na uwakilishi.
Mgombea Ubunge jimbo la Makunduchi, Wanu Hafidh Ameir, alisema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Tanzania inajivunia amani, utulivu na mashikamano.
Pia, mapinduzi katika sekta mbalimbali za kiuchumi, yameshuhudiwa hasa Sera ya Uchumi wa Buluu na ongezeko la ajira.
Pia, alisema mageuzi zaidi yamefanyika katika maisha ya watu na ustawi wa jamii kwa ujumla kama sekta ya afya, elimu na kuwezesha skuli za kusini kuingia katika 10 bora, mitihani ya taifa.
Kwa upande wake, Issa Haji Ussi ‘Gavu’ ambaye ni Mgombea Uwakilishi, Jimbo la Chwaka, alisema Chama Cha Mapinduzi, kimejiandaa kushinda kwa Tanzania bara na Zanzibar, kwa sababu mambo makubwa yanayowahakikishia ushindi huo ni umoja na mshikamano.
Gavu alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imetekeleza Ilani ya CCM kwa uhakika, kwa sababu hakuna kijiji, jimbo wala mtaa, ambao haujafikiwa maendeleo.
Alisema wapo watu wanaobeza na kuufanya uchaguzi huo wa kujifundishia, lakini CCM itaendelea kulinda na kudumisha amani iliyopo.
“Wanaopita wakapandikiza chuki, mifarakano na kuhubiri uchochezi, mjue kwamba hao wameishiwa kwani, hawana sera za kuzinadi, tuwakatae watu hao, sisi CCM hatuna muda tujiandae Oktoba 29, twende tukapige kura, tuna kila sababu ya kujivunia maendeleo yaliyoletwa na viongozi wanaotokana na Chama chetu,” alisema.




