Na MUSSA YUSUPH
MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, leo anatarajiwa kuanza mikutano ya kampeni za Uchaguzi Mkuu mkoani Mwanza.
Mikutano ya kampeni katika mkoa huo, inatarajiwa kuvutia wananchi wengi kutoka maeneo mbalimbali, ambapo wananchi wajawa shauku ya kumsikiliza Dk. Samia.
Mitaa ya mkoa huo, wenye utajiri wa samaki, imepambwa kwa mabango na picha mbalimbali, tayari kumpokea Dk. Samia ambaye anasifika kwa kutekeleza miradi mikubwa ukiwemo ujenzi wa Daraja la Kigogo – Busisi.
Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, alisema mbali ya Mwanza, Dk. Samia atafanya mikutano ya kampeni katika mikoa mingine ya Kanda ya Ziwa.
Aliitaja mikoa hiyo ni Shinyanga, Simiyu, Geita, Mara na Kagera.
Alisema katika mikoa hiyo, maendeleo mengi yamefikiwa ukiwemo ukamilikaji wa Daraja la Kigongo – Busisi (Daraja la Magufuli), kukamilika ujenzi wa chanzo cha maji cha Butimba, kinachowanufaisha wananchi 450,000 mkoani Mwanza.
Pia, alisema serikali, imefanikiwa kutekeleza mradi wa maji ya Ziwa Victoria, unaowahudumia wananchi 86,980 wa Tinde na Shelui.
“Ujenzi wa vivuko sita Ziwa Victoria, vimekamilika na kuanza kazi. Boti ya kuhudumia majeruhi wa ajali Ziwa Victoria. Chanjo ya mifugo imezinduliwa, sh. bilioni 62, zimetolewa,” alisisitiza.
Tangu kuanza kampeni za Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29 mwaka huu, Dk. Samia, ameendelea kuvutia maelfu ya Watanzania.
Hadi sasa, zaidi ya wananchi milioni 14.62, wamejitokeza katika mikutano 77, aliyofanya katika mikoa 21.
Pia, watu zaidi ya milioni 31.6, wamefuatilia mikutano hiyo ya kampeni iliyofanyika katika kanda za Kati, Magharibi, Pwani, Kusini, Nyanda za Juu Kusini, Pemba na Unguja (Zanzibar) na Kanda ya Kaskazini.
Kihongosi, alisema mahudhurio hayo makubwa, yameonesha namna Dk. Samia anavyokubalika kwa wananchi.
“Imani ya wananchi kwa Dk. Samia Suluhu Hassan, siyo bahati wala mkumbo, bali imechagizwa na uongozi wenye mafanikio makubwa katika miaka minne aliyoshika usukani wa Urais,” alisisitiza.
Kihongosi, alisema Dk. Samia, aliupokea mradi wa Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere (JNHPP), ukiwa asilimia 37 ambapo hadi sasa, umeanza kuzalisha umeme.
Vilevile, alisema Dk. Samia, amefanya vyema katika miradi ya miundombinu, kuanzia Reli ya Kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam mpaka Makutupora (kilometa 722), yaliyoleta mapinduzi makubwa ya usafiri wa treni kati ya Dar es Salaam na Dodoma.
“Ndani ya miaka minne ya uongozi wake, Dk. Samia, amejenga kilometa 15,366.36 za barabara.
“Chini ya uongozi wa Dk. Samia, ndege mpya sita za abiria na moja ya mizigo zimenunuliwa, hivyo kufanya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuwa na ndege 16.
Aliongeza: “Wananchi hasa wa vijijini, wamekuwa mashuhuda wa kazi kubwa ya Rais Samia.
“Miradi 1,633 ya usambazaji wa maji imekamilika, miongoni mwa hiyo , 1,335 ni ya vijijini peke yake.”




