Na MWANDISHI MAALUMU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kuwasisitiza Watanzania waendelee kuliombea Taifa, amani, upendo, ustahimilivu na mshikamano viendelee kudumu nchini.
Kauli hiyo ilitolewa mkoani Dodoma na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, alipowasilisha salamu za Rais Dk. Samia kwa waumini na viongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Kisasa.
“Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anawasalimu sana. Yuko pamoja nanyi na rai yake kwa Watanzania wote ni kuendeleza maombi kwa Taifa letu kuwa watulivu na kuiombea amani iendelee kudumu,”alisema.
Aidha, Waziri Mkuu, alisema kuwa, ni wajibu kwa kila Mtanzania, kuhakikisha amani ya nchi, inaendelea kulindwa na kuenziwa, kwa sababu pasipo amani, Taifa halitoweza kutekeleza majukumu yake, ikiwemo kufanya ibada na shughuli nyingine za kijamii.
“Pasipo amani, hatuwezi kutekeleza majukumu mengine yoyote, pasipo amani, hatuwezi kuendesha ibada. Hivyo, ni wajibu wa kila Mtanzania kuiombea nchi yetu.
“Pakiwa na amani, tunaweza kutekeleza yale yaliyo katika matarajio yetu, tunaweza hata kutatua yale tunayoyaona kuwa ni magumu,”alisema.
Ibada hiyo, iliongozwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Dodoma, Dk. Christian Ndossa, ambaye alitumia fursa hiyo kuwasisitiza Watanzania waishi kwa kumtanguliza Mwenyezi Mungu na wawe na matumaini kwake na wajiepushe na maovu.
Waziri Mkuu aliambatana na mkewe, Neema Nchemba, katika ibada hiyo.
Viongozi wengine waliohudhuria ibada hiyo ni Naibu Spika wa Bunge, Daniel Sillo, Mbunge wa Kilolo, Ritha Kabati, Mbunge wa Simanjiro, James Ole Millya, Mbunge wa Viti Maalumu, Balozi Dk.. Pindi Chana, Mbunge wa Itigi, Yohana Msita na Mbunge wa Kalenga, Jackson Kiswaga.




