Na MWANDISHI WETU
KONGAMANO kubwa zaidi duniani la kupambana na rushwa limemchagua Balozi Naimi Aziz, Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Umoja wa Mataifa (Vienna), kuwa Makamu wa Rais wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa dhidi ya Rushwa (UNCAC) kwa kipindi cha 2025–2027.
Uchaguzi huo umefanyika wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 11 wa Nchi Wanachama wa UNCAC uliofanyika Desemba 15, 2025, jijini Doha, Qatar.
Katika wadhifa huo, Balozi Naimi Aziz atamsaidia Rais wa Mkutano huo, Hamad bin Nasser Al-Misnad, ambaye pia ni Rais wa Mamlaka ya Udhibiti, Uwazi na Uwajibikaji ya Qatar, katika kuongoza mkutano huo.
Majukumu yake ni pamoja na kusimamia kazi za msingi za Mkutano Mkuu kama chombo kikuu cha kutunga sera za utekelezaji wa Mkataba, kuongoza vikao, kuandaa ajenda, kuwezesha majadiliano kuhusu utekelezaji wa UNCAC, pamoja na kushirikiana na Ofisi ya Rais katika mapambano ya kimataifa dhidi ya rushwa.
Mkutano huo umehudhuriwa na ujumbe wa Tanzania ulioongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Crispin Chalamila.
Viongozi wengine waliohudhuria ni pamoja na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, CPA Charles Kichere, pamoja na maafisa waandamizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma.
Wakati wa hafla ya ufunguzi, wito ulitolewa kwa nchi wanachama kutumia teknolojia zinazoibuka katika vita dhidi ya ufisadi, hususan katika kukabiliana na uhusiano wake na uhalifu uliopangwa pamoja na uhalifu mwingine wa kifedha.
Aidha, Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Annalena Baerbock, katika ujumbe wake alisema kuwa kuzuia na hatimaye kutokomeza rushwa ni jukumu la kila mtu, akisisitiza kuwa jamii ina deni kwa wananchi wanaowahudumia.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, katika ujumbe wake wa mtandaoni alisema rushwa si uhalifu usio na mwathirika, akibainisha kuwa inachochea migogoro, inaongeza ukosefu wa usawa na kupoteza rasilimali muhimu zinazohitajika kulinda watu na mazingira.
Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo unatarajiwa kuwasilisha ripoti ya utekelezaji wa Mkataba wa UNCAC kwa kipindi cha mwaka 2023 hadi 2025.





