Na MWANDISHI WETU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema Bima ya Afya kwa Wote, inatarajiwa kuzinduliwa Januari mwakani.
Aidha, Dk. Mwigulu, amezitaka hospitali zote nchini, zijiandae na bima ya afya kwa wote, wakiwemo, watoto, wanawake hususan wajawazito na wazee.
Alitoa maagizo hayo, alipozungumza na wananchi baada ya kukagua uharibifu wa miundombinu mbalimbali, ukiwemo mzani wa magari (Mpemba), Mahakama ya Mwanzo Tunduma na Soko la Machinga, katika ziara ya kikazi mkoani Songwe.
Dk. Mwigulu, alisema hatua hiyo ni sehemu ya ahadi za Rais Samia Suluhu Hassan, alizodhamiria kutekeleza katika kipindi cha siku 100 akiwa madarakani.
Alisema ahadi hizo, zinapaswa kuanza mara moja kama utoaji ajira za wahudumu wa afya 5,000, wauguzi na wakunga.
Alisema usaili wa wataalamu hao wa afya, ulianza Desemba 10, mwaka huu na unatarajiwa kukamilika wiki hii katika kila mkoa, ifikapo Januari, mwakani, wataalamu hao, watakuwa tayari katika majukumu yao.
“Ndani ya siku 100, walimu 7,000 watakuwa wameajiriwa, hivi tunavyoongea, usaili unaendelea kila mkoa kuajiri walimu hao, wakiwemo wa masomo ya sayansi, ifikapo Januari mwakani, walimu watakuwa wameajiriwa na kuendelea na majukumu ya kazi,”alisema.
Aidha, alitoa maelekezo kwa wasimamiaji wa usaili huo kuwa, hawapaswi kubagua mtu kwa itikadi ya udini, ukabila au kuwaweka ndugu zao katika ajira hizo, badala yake, wazingatie wenye sifa na uwezo wa fani hizo.
Vilevile Dk. Mwigulu, alisema kuanzia ndani ya siku 100 alizosema Rais Dk. Samia, kusiwe na hospitali inayozuia mwili wa marehemu kwa sababu ya ndugu kutokuwa na fedha za kulipa gharama.
“Naelekeza kila mkoa kufuatilia utekelezaji uliotolewa na Rais Dk. Samia na pasiwepo mtu anakataliwa matibabu kwa sababu, hajatoa fedha, nimesema mama mjamzito akifikia uchungu, aanzie kwanza na matibabu.
“Mtu yeyote aliyeletwa kwa dharura hospitalini, anapaswa kuanza kupatiwa matibabu, mambo ya uandikishaji yatakuja baadaye, lazima tuokoe maisha kwanza,”alisema.
Pia, Dk. Mwigulu, aliwatoa hofu wananchi kuwa, serikali itaendelea kutoa mitaji kwa vijana, wanawake na makundi maalumu, kufanya biashara kujikwamua kiuchumi.




