Na ELIZABETH JOHN
DIRA ya Maendeleo ya Taifa 2050 kupitia sekta ya viwanda na biashara, imeelezwa kuwa, mhimili mkuu wa kuijenga Tanzania ya uchumi wa kati, wa juu, shirikishi na yenye ajira nyingi.
Aidha, serikali imesisitiza kuwa, vijana ni nguvu kazi muhimu na walengwa wakuu wa mageuzi ya kiuchumi.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, aliyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema Dira ya 2050, inaweka mkazo katika maendeleo ya viwanda kama msingi wa kuongeza thamani ya rasilimali, kupanua wigo wa ajira, kupunguza uagizaji bidhaa kutoka nje na kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.
Alifafanua kuwa, kupitia sekta ya biashara, Dira hiyo inalenga kuimarisha ushiriki wa Tanzania katika masoko ya nje, ambapo thamani ya mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi, imeendelea kuongezeka, pamoja na jitihada za kupunguza nakisi ya biashara kwa kuongeza uzalishaji wa ndani na uongezaji thamani wa bidhaa.
Waziri huyo, alisema Dira ya 2050, inatambua sekta binafsi kama injini ya ukuaji wa uchumi, huku serikali ikiendelea kuwa mwezeshaji kupitia sera rafiki, sheria zinazochochea uwekezaji na miundombinu imara, kwa kuzingatia ushiriki wa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.
Akizungumzia utekelezaji wa Serikali ya Awamu ya Sita, waziri alisema katika kipindi cha miaka minne iliyopita, imefanya maboresho makubwa ya sera na sheria, kuboresha mazingira ya biashara, ikiwemo kuhuisha Sera ya Taifa ya Biashara, Sera ya Maendeleo Endelevu ya Viwanda na sera za kuendeleza wajasiriamali wadogo na wa kati.
Alisema maboresho hayo, yameanza kuleta matokeo chanya ikiwemo kuongezeka kwa mauzo ya nje ya bidhaa na huduma, hususan bidhaa za viwandani na kilimo zilizoongezwa thamani, sambamba na kupanuka kwa masoko ya kikanda kupitia Soko Huru la Biashara Afrika (AfCFTA).
Kwa mujibu wa waziri, sekta ya viwanda, imeendelea kuimarika, mchango wake katika pato la taifa umeongezeka, hali inayoonesha uimara wa uzalishaji wa ndani na ongezeko la thamani ya bidhaa zinazozalishwa viwandani.
Aliongeza kuwa, serikali imeendelea kufungua masoko mapya barani Afrika, Ulaya na Asia, hatua inayotoa fursa kubwa kwa Watanzania, hususan vijana, kushiriki katika biashara za kuuza nje bidhaa za kilimo, viwandani, mavazi na bidhaa nyingine zilizoongezwa thamani.
Katika kuboresha mazingira ya biashara, waziri alisema serikali imeimarisha mifumo ya kidijitali ya usajili na utoaji leseni kupitia BRELA na taasisi nyingine, hatua iliyorahisisha urasimishaji wa biashara na kuongeza idadi ya kampuni, majina ya biashara, leseni na hataza nchini.
Alieleza kuwa, juhudi hizo zimechangia kuongezeka kwa viwanda vipya, akitolea mfano Mkoa wa Pwani ambako ndani ya miaka minne viwanda vimeongezeka kwa zaidi ya 200, hali iliyoambatana na ongezeko la ajira.
Judith alibainisha kuwa, utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati kama Mchuchuma na Liganga, Magadi Soda Engaruka, Maganga Matitu na Katewaka unatarajiwa kuzalisha maelfu ya ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja, huku vijana wakiwa wanufaika wakuu.
Aidha, serikali imeendelea kuwekeza katika kongani za viwanda nchi nzima, zikiwemo Kwala na Mlandizi, ambazo zitatoa nafasi kubwa za ajira, ubunifu na biashara, pamoja na kuimarisha minyororo ya thamani ya uzalishaji.
Katika kuimarisha ujasiriamali, waziri alisema taasisi kama SIDO, TIRDO, TEMDO na CAMARTEC, zimeendelea kutoa mafunzo, teknolojia na huduma za uatamizi kwa vijana, sambamba na kuwaunganisha na masoko, viwango vya ubora na mitaji.
Alisema serikali imeongeza upatikanaji wa mikopo nafuu kupitia mifuko mbalimbali na benki za biashara kwa lengo la kuwawezesha vijana kuanzisha na kukuza viwanda vidogo, biashara za uzalishaji na ubunifu wa teknolojia.




