Na HANIFA RAMADHANI, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), inatarajia kutenga sh. trilioni moja kwa bajeti ijayo ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali.
Alisema sekta ya elimu ina mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi, hivyo lazima serikali itoa kipaumbele cha kwanza.
Rais Mwinyi, alisema hayo katika ufunguzi wa Shule ya Msingi Muungano Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, katika shamrashamra za maadhimisho ya miaka 62 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.
Alisema fedha hizo, zitaboresha miundombinu ya elimu, ukiwemo ujenzi wa shule za ghorofa, vifaa vya kisasa vya kujifunzia, kufundishia na kuimarisha matumizi ya teknolojia shule za msingi na sekondari.
Alisisitiza uwekezaji wa elimu msingi muhimu ni kwa maendeleo ya taifa na aliwataka wadau wa elimu, kushirikiana na serikali, watoto wapate elimu bora.
Akizungumzia teknolojia, Rais Mwinyi alisema serikali inatarajia kuwaandaa watoto mapema, kuwajengea uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya dunia.
Aliridhishwa na viwango vya ubora katika shule hiyo, ikiwa ndiyo ya kwanza ya ghorofa tatu kwa shule za msingi Zanzibar.
Alisema shule hiyo ina madarasa mazuri yenye samani za kisasa, hivyo wanafunzi watajifunza vyema.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Khamis Abdallah, alisema sh. bilioni 6.1, zimetumika kwa ujenzi wa shule hiyo ulioanza Mei, 2023.
Shule hiyo, ndiyo pekee yenye ghorofa tatu, ina madarasa 42, ofisi ya mwalimu mkuu, ofisi nne za walimu, ukumbi wa mitihani, maabara mbili na chumba cha TEHAMA.




