Na FRED ALFRED, Dodoma
TANZANIA imetajwa kuwa nchi ya pili Afrika Mashariki kwa kuwa na gharama ndogo za vifurushi vinavyotumika katika mitandao ya simu.
Kauli hiyo ilitolewa bungeni jijini hapa na Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dk. Switbert Mkama, alipojibu swali la nyongeza la Condester Sichalwe Mbunge wa Momba- CCM).
Mbunge huyo alitaka kujua mkakati wa serikali kukaa na watoa huduma za intaneti kutoka taasisi binafsi kupunguza gharama za vifurushi.
Akijibu swali hilo, Dk. Mkama alisema serikali tayari ilishakaa na watoa huduma hao na kupunguza bei za vifurushi.
“Hivi sasa ukiondoa nchi ya Rwanda, Tanzania ndiyo nchi yenye vifurushi nafuu zaidi kuliko nchi nyingine zote. Tutaendelea kukaa na taasisi binafsi kuangalia namna ambavyo tunaweza kuboresha zaidi kupungua kwa gharama za vifurushi kufikia uchumi wa kidijiti,” alisema.
Katika hatua nyingine, Dk. Mkama alisema serikali inatambua umuhimu wa upatikanaji huduma za mawasiliano kwa gharama nafuu.
Alisema wizara kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) na Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), imeendelea kuchukua hatua kuhakikisha huduma za simu, intaneti na data zinakuwa na bei rafiki kwa wananchi.
“Hatua zilizochukuliwa ni kusimamia ushindani wa haki miongoni mwa kampuni za simu kuchochea ubunifu na upatikanaji vifurushi vya gharama nafuu vinavyokidhi uwezo wa wananchi, kufanya mapitio ya gharama na tozo mbalimbali kuhakikisha utozaji unazingatia gharama halisi za huduma na kumlinda mlaji wa mwisho,” alisema.
Naibu Waziri huyo alisema hatua nyingine ni kuhimiza matumizi ya miundombinu ya pamoja kwa kupunguza gharama za uendeshaji, kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya mawasiliano maeneo ya vijijini, maeneo yasiyo na mvuto wa kibiashara na ujenzi wa vituo vya kuhifadhi data.
Kwa mujibu wa Naibu waziri huyo, hatua hiyo inachangia kushuka kwa gharama za huduma hususan intaneti ya faiba nyumbani na ofisini.



