Na NASRA KITANA
WACHEZAJI wa Yanga wamekiwa kutumia nafasi watakazopata katika mchezo dhidi ya FAR Rabat ya Morocco kushinda pambano la hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Yanga itakuwa ugenini keshokutwa kupambana na FAR Rabat katika mchezo utakaochezwa Uwanja wa Stade Olympique, Rabat kianza saa 4:00 usiku.
Katika mchezo huo, Yanga inatakiwa kushinda kufuzu hatua ya robo fainali ya michuano.
Kuelekea mchezo huo, baadhi ya wachambuzi wa soka wametoa maoni yao kuhusu mchezo huo.
Kiongozi na mchezaji wa zamani wa Yanga na kocha wa Ruvu Shooting, Charles Mkwasa alisema kuwa anajua hautakuwa mchezo rahisi kwao lakini Yanga wanatakiwa kufanya mashambilizi ya mapema.
“Wanatakiwa kupambana kwa jasho na damu lakini kupata mabao ya mapema katika kipindi cha kwanza, lengo wakirejea kipindi cha pili wazuie magoli,” alisema Mkwasa.
Naye mchambuzi wa masuala ya soka chini, Kennedy Mwaisabula alisema Yanga huo ni mchezo wa kufa au kupona hivyo wanatakiwa kutumia nguvu zao zote kupata ushindi.
“Ni muhimu Yanga kupata ushindi katika mchezo huu, hivyo wachezaji wanatakiwa kujitoa kwa jasho na damu kupata ushindi na wanatakiwa kila nafasi wanayoipata waitumie vizuri,” alisema Mwaisabula.
Nyota wa zamani wa Simba, Boniface Pawasa alisema kwanza Yanga wanatakiwa kupongezwa kwa kazi kubwa waliyoifanya.
“Kubwa ambalo Yanga wanatakiwa kufanya ni kushinda magoli mengi ya mapema ili kipindi cha pili wazuie magoli waliyoyapata,” alisema Pawasa.
Nyota wa zamani wa Simba na Yanga, Zamoyoni Mogella alisema wachezaji wa Yanga wanatakiwa kufuata kile ambacho mwalimu atawafundisha.
“Sina shaka na Yanga katika suala la kupambana, ninachoweza kuwaambia wanatakiwa kufuata kile ambacho mwalimu amewafundisha kutimiza malengo waliojiwekea,” alisema Mogella.
Kwa sasa, msimamo wa Kundi B wa Ligi ya Mabingwa Afrika unaongozwa na Al Ahly yenye pointi 8, ikifuatiwa na Yanga yenye pointi 5 sawa na FAR Rabat huku JS Kabylie ikiwa na alama mbili.




