Na NASRA KITANA
WAKATI timu ya Simba ikiwa imepoteza nafasi yake ya kutinga hatua robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, siri imevuja kuwa klabu hiyo imekiri kuwa msimu huu haikuwa na kikosi bora.
Akizungumza na UHURU Dar es Salaam, mmoja wa viongozi wa klabu hiyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake, amesema msimu huu timu yao bado haipo vizuri.
“Amesema hata kutinga hatua ya makundi ya mashindano hayo ilikuwa kwa mbinde,,”alisema.
Kiongozi huyo alisema baada ya kumaslizika mashindano hayo ya kimataifa, watafanya tathimini ya kikosi hicho na kukirekebisha ili kiibuke na ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho (FA).
“Tumekosa nafasi mwaka huu, timu yetu haikuwa sawasawa na hii haijaanza katika mechi dhidi ya Esperance de Tunis tu, ukiiangalia safari yetu tangu tumeanza Ligi ya Mabingwa Afrika tumekuwa na mwendo wa kusuasua.
“Katika mechi zetu mbili zilizobakia tutahakikisha tunashinda zote kuweka heshima, lakini sasa nguvu na akili zetu zote tutazielekeza katika mechi zetu za Ligi Kuu pamoja na FA,” alisema.
Kiongozi huyo alifafanua kuwa mashabiki na wapenzi wa Simba huu siyo muda wa kulaumiana bali kuungana kwa pamoja ili timu yao iweze kufikia malengo waliojiwekea.
“Nadhani watu wameona juhudi za viongozi kipindi hiki cha dirisha dogo la usajili, tumefanya usajili mzuri, wachezaji wote tuliowasajili wameonesha uwezo mkubwa, ” alisema kiongozi huyo.
Alisema kuwa umoja na mshikamno ndio nguzo pekee itakayowasaidia wachezaji kufanya vizuri katika mechi za ligi na FA.
Simba ilianza michuano hiyo Septemba 20 mwaka jana iliposhinda bao 1-0 ugenini dhidi ya Gaborone United ya Botswana, kabla ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 nyumbani, Septemba 28 mwaka jana katika mechi ya hatua za awali.
Katika raundi ya kwanza ilishinda ugenini mabao 3-0, Oktoba 19 mwaka jana, kabla ya kulazimishwa suluhu nyumbani, Oktoba 28 mwaka jana.
Baada ya kutinga hatua za makundi ilikutana na kipigo cha bao 1-0 nyumbani dhidi ya Petro de Luanda, mabao 2-0 ugenini dhidi ya Stade Malien ya Mali, kabla ya Jumapili iliyopita kulazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya Esperance de Tunis.
Simba inashika mkia katika Kundi D, ikiwa na pointi moja baada ya kucheza mechi nne, ikipoteza tatu na sare moja huku Stade Malien ikiongoza kundi hilo ikiwa na point nane, akifuatiwa na Esperance yenye pointi sita huku Petro de Luanda ikiwa nafasi ya tatu na pointi tano.




