Na ATHNATH MKIRAMWENI
MAKAMU wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, ametoa wito kwa sekta binafsi kushirikiana na vyuo, kuwekeza katika utafiti hususan za sayansi na teknolojia ili kuinua viwango vya tafiti na ubora wa elimu nchini.
Makamu wa Rais, alisema hayo katika uzinduzi wa mpango wa ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Waajiri, uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam.
Alisema kupitia mpango huo, sekta binafsi inaweza kuchangia maendeleo ya elimu kwa kufadhili tafiti na kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa fani mbalimbali kulingana na mahitaji ya soko la ajira.
Aidha, Makamu wa Rais, alitoa wito kwa taasisi za elimu na sekta binafsi nchini, kuzingatia maendeleo ya kasi ya sayansi na teknolojia duniani katika utekelezaji wa mpango huo.
Alisema kuwa, vyuo na sekta binafsi, vishirikiane kubaini ujuzi muhimu unaohitajika sasa na siku zijazo hususan katika fani za sayansi, teknolojia, ubunifu, tiba, uhandisi na hesabu ili kuwezesha vijana kushindana na kupata nafasi katika soko la ajira nchini na kimataifa.
Alisema ushirikiano baina ya Taasisi za elimu na viwanda, ni hitaji la lazima katika dunia ya leo, kwa kuwa vyuo haviwezi kuwa visiwa vya nadharia, na viwanda haviwezi kukua bila nguvukazi yenye ujuzi unaoendana na teknolojia na ushindani wa soko.
Aliongeza Serikali ya Awamu ya Sita, imeweka kipaumbele cha kimkakati katika kukuza ujuzi, stadi, maarifa na sifa za kuajirika au kujiajiri miongoni mwa vijana na wahitimu wa ngazi mbalimbali za elimu.
Alisema serikali imeendelea kufanya maboresho makubwa ya sera na mitaala ya elimu katika ngazi zote kwa lengo la kuujenga mfumo wa elimu ulio mnyumbufu, jumuishi na unaoendana na vipaji, mwelekeo na mahitaji halisi ya soko la ajira, huku ikizingatia mabadiliko ya teknolojia na ushindani wa kitaifa na kimataifa.
Uzinduzi wa Mpango huo ni utekelezaji wa ahadi ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, alioitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2025, ambapo aliahidi kuanzisha mpango wa pamoja kati ya waajiri, vyuo vya ufundi stadi na vyuo Vikuu kwa lengo la kulinganisha mafunzo na mahitaji halisi ya sekta za kipaumbele za Taifa, ndani ya siku 100 baada ya kuapishwa kwake.
Mpango wa ushirikiano kati ya Taasisi za Elimu na Viwanda, unalenga kuimarisha uhusiano wa kimkakati kati ya utoaji wa elimu na utendaji kazi, kwa lengo la kulinganisha mafunzo na mahitaji ya sekta za kipaumbele kama nishati, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na viwanda vya kuongeza thamani.
Aidha, mpango unaweka msingi thabiti wa kujenga kizazi cha wahitimu wenye uwezo wa kuajirika, kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwani umedhamiria kubadilisha mfumo wa elimu ya nadharia kwenda mfumo unaozingatia ujuzi, vitendo, ubunifu na uzalishaji mali.
Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia itaendelea kushirikiana na wadau wanaohusika katika Mpango huo kuhakikisha unaleta tija katika sekta ya elimu na ajira hususani kwa vijana.
Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, alisema serikali imejizatiti kuhakikisha nchi inazalisha rasilimali watu yenye ujuzi, unaokidhi mahitaji halisi ya soko la ajira ili kufanikisha Ajenda ya Uchumi wa Viwanda.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU
Naye Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, alisema ushirikiano kati ya taasisi za elimu, sekta ya uzalishaji na waajiri ni wajibu wa mifumo ya elimu na si hiari, kwa mujibu wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Taifa.




