Na Asnath Mkilamweni
KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, amejitosa kutatua mgogoro wa ardhi wilayani Nzega, mkoani Tabora ambao umedumu kwa miaka 30.
Amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Nzega mkoani humo, Naitapwaki Tukai, kuchunguza na kuumaliza mgogoro huo wa ardhi kati ya Richard Charles na majirani zake uliozuka mwaka 1996.
Kihongosi ambaye yuko ziarani Tabora, alitoa maagizo hayo baada ya kusikiliza kero za wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Stendi ya Zamani, Nzega.
Akizungumzia mgogoro huo kati ya mwananchi huyo na majirani zake uliodumu miaka 30, Kihongosi alimtaka mkuu wa wilaya hiyo kutenda haki katika kushughulikia mgogoro huo unaohusisha eneo linalogombaniwa.
Katibu mwenezi huyo wa CCM Taifa, alimsisitiza Tukai kuhakikisha anajiridhisha kwa ushahidi wa pande zote katika kutafuta ufumbuzi wa sakata hilo la ardhi.
Maagizo hayo ya Kihongosi yalitokana na Charles kudai kwamba, mwaka 1996 mahakama ya wilaya ilifuta kesi dhidi yake ya kugombea ardhi na hata ilipofunguliwa tena 2010, alishinda, lakini serikali ya kijiji haikumpa haki yake.
ATOA SIKU 14
Pamoja na hayo, kiongozi huyo aliipa siku 14 ofisi ya ardhi wilayani Nzega, kutatua migogoro iliyopo na kuwachukulia hatua za kisheria viongozi wa serikali za mitaa wanaoisababisha.
Alisema baadhi ya viongozi wamekuwa wakisababisha migogoro kwa kuchukua rushwa kutoka kwa watu wanaonunua maeneo, hivyo kusababisha eneo moja kuuzwa kwa mtu zaidi mmoja.
“Baadhi ya watu wanatengeneza migogoro makusudi kwa kupokea rushwa, fuatilieni msiishie tu kuangalia mkasema kuna wamiliki wawili, Selemani aoneshe mipaka yake na huyo mama aoneshe mipaka ukweli ujulikane,” alisema.
Kihongosi alifikia hatua hiyo baada ya mkazi wa Nzega, Fatuma Abdallah kudai amedhulumiwa eneo lake na kijana anayefahamika kwa jina la Seleman, ambaye ni jirani yake aliyeuza eneo lake kwa watu wawili, japokuwa mwenyekiti wa eneo hilo alidai hamtambui mama huyo.
Fatuma alidai alisafiri kwenda mkoani Dar es Salaam kumuuguza binti yake, lakini aliporudi alikuta eneo lake limevamiwa na kuelezwa Selemani ndiye aliyewauzia watu hao, akidai ndiye mmiliki halali.
Baada ya maelezo hayo, Kihongosi alimtaka kamishna msaidizi wa ardhi kujiridhisha mmiliki wa halali wa eneo hilo na kwa waliouziwa wajiridhishe waliuziwa na nani na kama uongozi wa serikali ya mtaa umehusika, uchukuliwe hatua za kisheria.
Katika mkutano huo, Kihongosi alitatua kero zaidi ya 40 kuhusu masuala ya ardhi, fidia, huduma za afya, barabara na umeme kwa wakazi wa Nzega.
AITAKA WIZARA KUKAMILISHA UJENZI WA CHUO CHA VETA
Katika hatua nyingine, Kihongosi ameielekeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kuharakisha utoaji fedha za kukamilisha ujenzi wa chuo cha ufundi stadi (VETA) wilayani Nzega, kianze kuhudumia wananchi.
Mradi huo unatekelezwa kwa gharama ya sh. milioni 500, huku zaidi ya sh. milioni 400 zikiwa zimeshatumika.
Kihongosi alisema ameridhishwa na ubora wa majengo ya VETA, zikiwemo karakana, jengo la utawala na miundombinu mingine na kusisitiza thamani ya fedha ionekane kulingana na kazi iliyofanyika.
“Ninaielekeza Wizara ya Elimu kuhakikisha fedha za ukamilishaji wa ujenzi zinaletwa haraka wananchi waanze kunufaika na uwekezaji huu,” alisema Kihongosi.
Alibainisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amekuwa akielekeza miradi yote ya maendeleo ikamilike kwa wakati wananchi wapate huduma stahiki, hivyo hakuna sababu ya kuchelewesha ujenzi wa chuo hicho.
Kihongosi alisema kukamilika chuo cha VETA kutakuwa mkombozi kwa vijana wengi watakaopata mafunzo ya ufundi stadi kwa fani za useremala, uchomeleaji, umeme na udereva, jambo litakalowawezesha kujiajiri na kuinua uchumi wao, wilaya, mkoa huo na taifa kwa ujumla.
Alifafanua chuo hicho kitawapa fursa wahitimu wa darasa la saba, kidato cha nne, sita hadi ngazi ya shahada, kujiunga na kupata ujuzi wa ziada utakaowaongezea thamani katika soko la ajira.
Katibu huyo wa uenezi taifa, aliwasisitiza wananchi wa Nzega kuilinda miundombinu ya miradi mbalimbali kwa kuhakikisha vifaa vilivyojengewa haviibiwi kwa manufaa ya vizazi vya hivi sasa na baadaye.
Kwa upande wake msimamizi wa mradi wa VETA, Nicodemus Shirima alisema hadi hivi sasa, majengo tisa yamejengwa, likiwemo la utawala, chumba cha mlinzi na karakana tatu za ufundi bomba, umeme, mapishi na useremala.
Alisema ujenzi umefikia asilimia 75, lakini changamoto kubwa iliyopo ni upungufu wa fedha na kubainisha zikipatikana kwa wakati mradi huo utakamilika mapema.
Ziara ya Kihongosi mkoani Tabora inalenga kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kuhakikisha fedha za umma zinatumika ipasavyo pamoja na kusikiliza changamoto za wananchi.




