Na MWANDISHI WETU, Ruvuma
WAPIGA Kura 127,632 walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, watashiriki uchaguzi wa kuchagua mbunge wa Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea, Mkoa wa Ruvuma na Kata ya Shiwinga, iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoa wa Songwe.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufaa, Jacobs Mwambegele, alisema hayo mjini Songea, akisoma risala kuhusu uchaguzi katika jimbo na kata husika utakaofanyika leo ambapo vituo 373 vya kupigia kura, vitatumika.
“Kati yao, wapigakura 120,780 ni wa Jimbo la Peramiho na wapigakura 6,852 wapo katika Kata ya Shiwinga na jumla ya vituo 373 vya kupigia kura vitatumika.
“Vituo 354 vipo Jimbo la Peramiho, vituo 19 vipo Kata ya Shiwinga Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi,”amesema Jaji Mwambegele.
Aidha, alisema kwa uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Peramiho, vyama vya siasa 15, vimesimamisha wagombea na uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Shiwinga, vyama vya siasa vinane vimesimamisha wagombea.
“Natumia fursa hii kuvikumbusha vyama vya siasa vinavyoshiriki uchaguzi, kuzingatia wajibu wao wa kuweka mawakala katika vituo vyote vya zoezi la kupiga, kuhesabu na kujumlishia kura.
“Wasimamizi wa uchaguzi katika Jimbo na Kata husika, wamekamilisha utaratibu unaoweka mazingira yanayowawezesha mawakala wa vyama vya siasa, kufuatilia mchakato mzima wa uchaguzi,”alisema Jaji Mwambegele.
Alisema mawakala hao, wanawajibika kulinda maslahi ya vyama na wagombea wao, hivyo, wanapaswa kuzingatia sheria, kanuni, utaratibu wa uchaguzi na maelekezo ya Tume katika utekelezaji wa majukumu yao vituoni.
“Vituo vitafunguliwa saa 1:00 asubuhi, kufungwa saa 10:00 jioni na ifikapo muda wa kufunga kituo saa 10:00 kamili jioni, kama wapigakura bado wapo katika mistari, mlinzi wa kituo, atasimama nyuma ya mtu wa mwisho na zoezi la upigaji kura litaendelea hadi wapigakura walio kwenye mstari watakapomalizika
“Baada ya kumaliza kupiga kura, mpigakura anatakiwa kuondoka eneo la kituo cha kupigia kura na mpigakura awapo kituoni, anatakiwa kufuata maelekezo yote atakayopewa na karani mwongozaji wapigakura,”alisema Jaji Mwambegele.
Jaji Mwambegele alisema mpiga kura ambaye ameandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapigakura na taarifa zake zipo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililopo katika kituo husika, lakini amepoteza kadi au kadi yake imeharibika, ataruhusiwa kupiga kura kwa kutumia moja wapo ya vitambulisho cha Taifa NIDA, leseni ya udereva au pasi ya kusafiria (passport).




