Na MWANDISHI WETU
WAKATI Kocha wa Azam FC, Florent Ibenge akiweka wazi hatua ya kikosi chake kushindwa kutengeneza nafasi za kufunga ndiyo sababu ya kutoshinda, Pedro Goncalves wa Yanga amesema uchovu wa wachezaji wake ni miongoni mambo yaliyochangia kukosa pointi tatu dhidi ya wapinzani wake hao juzi.
Azam FC na Yanga zilitoka sare juzi katika mchezo wa dabi ya Ligi Kuu Tanzania Bara maarufu Dar es Salaam Dabi uliopigwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Katika mtanange huo uliokuwa na ushindani wa aina yake, asilimia kubwa ya mpira ulikuwa ukichezwa katikati ya uwanja huku timu zote zikishindwa kutengeneza nafasi za wazi kuandika mabao.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Kocha Ibenge alisema Azam FC ilianza vyema kipindi cha kwanza kwa kutawala mechi lakini sababu kubwa ya kutoandika bao ni kukosa umakini wa kutengeneza nafasi za wazi.
Ibenge alisema lengo lake lilikuwa ni kuvuna pointi tatu, lakini kushindwa kutengeneza nafasi za wazi ilikuwa sababu tosha ya kutofunga bao.
“Tulianza vizuri na tulikaa vyema na mpira, lakini bahati mbaya tulishindwa kutengeneza nafasi za mabao.
Hongera kwa Yanga kwa kutulazimisha sare nyumbani, lakini sasa tuna kazi kuhakikisha tunakwenda Kigoma (dhidi ya Mashujaa) kuwania pointi tatu,” alisema.
Kocha wa Yanga, Pedro alisema ilikuwa mechi ngumu, lakini uchovu wa wachezaji wake baada ya kucheza mechi mfululizo, ilichangia kutokuwa bora uwanjani.
“Ilikuwa mechi ngumu, tulikuwa na ratiba ngumu, kama tungepata muda wa kupumzika zaidi kabla ya mechi hii, ninafikiri tungekuwa bora zaidi.
Tunachukua pointi moja tuliyopata, najua siyo tulichokuwa tunapambania lakini tunaichukua hii na kujielekeza zaidi katika mechi ya Jumatano (kesho),” alisema.
Kuanzia Februari 22 hadi juzi ambapo ni sawa na siku 22, Yanga imecheza jumla ya mechi sita za Ligi Kuu Bara ambazo ni sawa siku nne kila baada ya mechi moja (ukiondoa mechi za FA).
Katika siku hizo, Yanga ilishinda mechi nne dhidi ya Namungo (1-0), JKT Tanzania (5-0), Singida Black Stars (3-0) na Tanzania Prisons (1-0) na kutoka sare dhidi ya Simba (0-0) na Azam FC (0-0).
Yanga ndiyo kinara wa ligi hiyo ikiwa na pointi 36 baada ya kushuka dimbani mara 14 ikifuatiwa na Azam FC yenye alama 28 katika mechi 14.




