Na Mwandishi Wetu
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amewataka wakaguzi wasaidizi wa madini kutekeleza majukumu kwa ubunifu, uzalendo na uadilifu ili sekta ya madini iendelee kutoa mchango mkubwa kwa ukuaji wa uchumi wa taifa.
Amesema madini ni miongoni mwa sekta zilizopewa kipaumbele katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hivyo usimamizi madhubuti wa rasilimali za madini ni muhimu kufanikisha malengo ya ya nchi.
Akizungumza wiki hii, wakati wa kikao cha menejimenti ya Tume ya Madini na wakaguzi wasaidizi wa madini nchini, kilichofanyika mkoani Morogoro, Mhandisi Samamba amewataka kusimamia rasilimali za madini kwa uzalendo.
Aidha, amewasisitizia kujiepusha na rushwa, akieleza kuwa sekta ya madini ina vishawishi vinavyoweza kuathiri utendaji kazi na kuonya kwamba serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria dhidi ya yeyote atakayebainika kujihusisha na uhalifu huo.
Katika hatua nyingine, Mhandisi Samamba amewataka wakaguzi wasaidizi wa madini kushirikiana kwa karibu na mamlaka zingine za Serikali kuanzia ngazi ya vijiji, kata, wilaya na mikoa ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu yao na utatuzi wa changamoto zinazoweza kujitokeza katika maeneo yao ya kazi.
“Sambamba na ushirikiano huo, ninawataka kuhakikisha mnatoa huduma bora na kwa wakati kwa wananchi wanaojihusisha na shughuli za madini ili kuendelea kujenga taswira chanya ya sekta ya madini na kuongeza imani ya wananchi kwa serikali yao,” amesema Mhandisi Samamba.
Pia, amewataka viongozi na watendaji wa Tume ya Madini kuendelea kutoa mafunzo kwa wakaguzi wasaidizi wa madini, hususan katika sheria, kanuni na taratibu za madini ili kuwawezesha kutekeleza majukumu kwa ufanisi.
Wakati huo huo, Mhandisi Samamba amepongeza mchango wa wakaguzi wasaidizi wa madini katika kuimarisha usimamizi wa sekta hiyo, hatua iliyochangia ongezeko la makusanyo ya maduhuli pamoja na kupungua kwa ajali katika maeneo ya migodi.
“Kwa mfano, katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi sasa, Tume ya Madini imefanikiwa kukusanya sh. trilioni 1.36, sawa na asilimia 113.34 ya lengo la makusanyo kwa mwaka wa fedha 2025/2026, huku ninyi mkiwa sehemu muhimu ya mafanikio hayo kupitia kazi zenu za ukaguzi na usimamizi wa shughuli za madini,” amesema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Dkt. Venance Mwasse, akizungumza kwa niaba ya Wakuu wa Taasisi zilizopo chini ya wizara ya madini pamoja na Kamishna wa Madini, Dk. Abdulrahman Mwanga, wamewapongeza wakaguzi wasaidizi wa madini kwa mchango wao katika maendeleo ya sekta hiyo.
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dk. Janet Lekashingo, ameishukuru wizara hiyo kwa kuendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa kutoa vifaa vya kazi; magari na mashine za kisasa za kupima madini ya metali.



