Na MWANDISHI MAALUMU, Zanzibar
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) katika kutumia uhamaji kuchochea maendeleo, uwekezaji na fursa salama za ajira.
Alisema hayo Ikulu Ndogo Zanzibar, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa IOM, Amy Pope, aliyeko nchini kwa ziara ya kikazi.
Katika mazungumzo hayo, viongozi hao, walijadili namna bora ya kuoanisha vipaumbele vya IOM na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan katika masuala ya ajira, diaspora, uwekezaji, usimamizi wa mipaka na kuimarisha usalama wa afya nchini.
“Tuna nafasi nzuri ya kujenga ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na IOM, kwa kuandaa programu zinazoendana na Dira yetu ya Maendeleo 2050 na mahitaji halisi ya wananchi,” alisema.
Alisema Tanzania ipo tayari kutumia maarifa, ujuzi, mitaji na mitandao ya diaspora, kuharakisha maendeleo kwa kuwawezesha Watanzania wafanyao kazi nje ya nchi, kuwekeza nyumbani na kutumia uzoefu walioupata katika kuchangia uchumi wa taifa wanaporejea nchini.
Rais Samia alisema ushirikiano huo, unapaswa pia kuimarisha mifumo ya ajira nje ya nchi, kuwawezesha Watanzania kupata kazi zenye staha kwa njia salama, mikataba yenye maslahi na ulinzi dhidi ya unyonyaji.
Alieleza kuwa, Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanakotoka wahamiaji, wanakopita na wanakoelekea, kudhibiti uhamaji usio wa kawaida kwa kuzingatia misingi ya sheria, utu, na usalama wa taifa.
Vipaumbele vingine ni kuandaa sera jumuishi ya taifa ya uhamiaji, kuboresha uratibu na takwimu za wahamiaji, kutumia teknolojia katika usimamizi wa mipaka, kukabiliana na uhamaji unaosababishwa na majanga pamoja na mabadiliko ya tabianchi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa IOM, Amy alisema shirika hilo, lipo tayari kuisaidia Tanzania kutumia uhamaji kuchochea maendeleo kwa kuwaunganisha vijana na fursa halali za ajira duniani, mafunzo ya ujuzi na uwekezaji wenye manufaa ya muda mrefu nchini.
“Dunia inahitaji wahamiaji, Tanzania ina vijana wanaohitaji fursa. Tunataka kuhakikisha uhamaji unaleta uwekezaji, ukuaji na ujuzi, huku tukiwalinda wanaotafuta ajira nje ya nchi dhidi ya unyonyaji na ukiukwaji wa haki,” alisema.
Aliongeza kuwa, IOM inaweza kuisaidia Tanzania kuifikia jumuiya ya diaspora, kutambua ujuzi ilionao na kuweka mifumo ya uwekezaji pamoja kuimarisha usimamiziwa mipaka, utambulisho, afya na usalama katika maeneo rasmi ya kuingia nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa IOM, Amy alitahadharisha kuhusu hatari ya mitandao inayowalaghai vijana wa Afrika kwa ahadi za ajira nje ya bara hilo.
Alisisitiza umuhimu wa upatikanaji wa taarifa sahihi, mikataba salama ya ajira na ulinzi wa kutosha wa waombaji kabla ya kuondoka katika nchi zao.
Pia, alisema viongozi hao walijadili ushirikiano katika matumizi ya nishati safi ya kupikia wakati wa dharura za kibinadamu, hususan katika kulinda afya na usalama wa wanawake,
kuhifadhi mazingira na kuimarisha uwezo wa jamii kukabiliana na majanga.




