Na FRED ALFRED, Dodoma
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa msisitizo kwa viongozi nchini, kutambua nafasi walizopewa ni dhamana ya kuwahudumia wananchi, siyo kujinufaisha wala kuvimba.
Rais Samia, alitoa msisitizo huo katika hafla ya kuwaapisha viongozi aliowateua hivi karibuni iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma jana.
Alisema vyeo ni dhamana kutoka kwa Mungu, hivyo vinapaswa kutumika kwa uadilifu na manufaa ya jamii.
“Vyeo ni dhamana. Ni dhambi kubwa ukikipata kuvimba mabega.
“Wewe ni kiumbe kama wengine, ila Mungu ameamua ushike nafasi hiyo kwa lengo la kuwatumikia watu ukiwa duniani,” alisema Rais Dk. Samia.
Aliongeza: “Usipotumikia watu, Mungu ana adhabu yake na serikali inapitia tu. Kwa hiyo, nawaombea mfanyekazi kwa bidii.”
ATAJA SIRI YA KUMTEUA MUNISI
Rais Samia alitaja sababu za kumteua aliyekuwa Mgombea urais kupitia Chama cha NCCR – Mageuzi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025, Evaline Munisi, kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano.
Alisema amemteua Evaline kwa sababu ya uchapakazi, uzalendo, hivyo ana sifa ya kuingia serikalini kusaidia masuala mbalimbali.
“Evaline ni Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR-Mageuzi, lakini nimeangalia wasifu wake, nimeona ana sifa ya kuingia serikalini na kutusaidia.
“Sote ni Watanzania, tunatakiwa kuongeza nguvu ili twende pamoja.” alibainisha.
Alimtaka kuhakikisha sheria za kazi nje ya nchi zinafuatwa na kutafuta fursa za ajira kwa vijana.
“Vilevile, nakutaka ukaimarishe mahusiano kati ya serikali na makundi mbalimbali na kuongeza ukaribu kati ya serikali, waajiri na waajiriwa,” alisisitiza Rais Dk. Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia, alisisitiza suala la kuheshimiana mahali pa kazi, huku akihimiza kila mtu kutimiza wajibu wake.
Kuhusu uteuzi wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Kheri Mahimbali, alisema lengo ni kuifufua upya taasisi hiyo kuifanya kuwa chombo imara cha serikali.
Alisema ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), imeonesha TEMESA haijasimama vizuri huku kukiwa na maswali mengi yasiyojibika.
“Nimekuteua ukasimamie TEMESA na kuifanya kuwa chombo cha serikali kinachotumainika. TEMESA hivi sasa ukipeleka gari, unaambiwa hawana vifaa, unapewa ruhusa ya kupeleka nje.
Alibainisha: “Ukiangalia CAG ametaja mapungufu mengi, naomba ukashirikiane na waziri wako, mkasimamie na kuitengeneza TEMESA kuwa chombo imara cha serikali.”
Pia, alisema amemteua Peter Mwasalyanda kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), akiamini atafanya kazi kubwa yenye mafanikio.
Aidha, alisema amempa muda wa miezi sita kwa uangalizi kabla ya kumthibitisha kupima uwezo wake.
Kuhusu uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) Dk. Jabir Bakari, alisema ni kwa sababu ya kazi nzuri aliyoifanya alipokuwa TCRA.
Alisema TCAA ni sekta muhimu kwa usalama wa nchi na wananchi wanaosafiri kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
“Nenda ukaendelee kufanya kazi katika sekta hii muhimu kwa nchi yetu, naamini utafanya hayo.”
Kuhusu mabadiliko ya makatibu wakuu, Rais Samia, alisema ni ya kawaida huku akisisitiza wafanyekazi kwa bidii.



