Na MWANDISHI WETU, Bukoba
UNAWEZA kusema ni shangwe baada ya timu ya Simba kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Kagera Sugar.
Mashabiki wa klabu hiyo, mkoani Kagera, jana walipokea kwa furaha ushindi huo, baada ya wiki iliyopita timu yao kupokea kipigo cha 1-0 kutoka kwa watani wao wa jadi, Yanga katika mchezo wa Ngao ya Jamii.
Katika pambano hilo la jana, lililopigwa katika Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba ukiwa ni mchezo wa kwanza wa Ligi kuu Tanzania Bara msimu wa 2026/27 kwa timu hizo, mashabiki wa Simba waliwashangilia wachezaji wao muda wote wa mchezo huo.
Simba ilishinda pambano hilo, ikiwa pungufu, baada ya David Kameta ‘Duchu’ kutolewa kwa kadi nyekundu na mwamuzi Saad Mrope kutoka Dodoma, dakika ya 55 baada ya kucheza rafu kwa mchezaji wa Kagera Sugar.
Bao la kwanza la Simba, lilipachikwa wavuni na Ismael Toure katika dakika 45 ya mchezo huo.
Toure alimalizia mpira wa kona uliopigwa na Libasse Gueye.
Dakika ya 69, Simba walipata bao la pili, kupitia kwa Elie Mpanzu ambaye alifumua shuti kali na mpira kuingia kambani.
Mpanzu aliyeingia kipindi cha pili akichukua nafasi ya Ibrahim Doumbia alipamilizia pasi safi kutoka kwa Gueye.
Awali, mchezo huo ulianza kwa kasi ambapo dakika ya 10 ya mchezo, Simba walikosa bao kupitia kwa mchezaji wake, Ibrahim Doumbia ambaye alipiga shuti kali na mpira kutoka nje.
Dakika ya 78 Kagera Sugar walikosa bao, baada ya Hassan Mwaterema kupiga shuti kali nje ya 18 na mpira ulitoka nje ya lango.
Katika dakika ya 83, Simba walifanya mabadiliko aliingia kipa, Hussein Abel kuchukua nafasi ya Mahamadou Kassali baada ya kupata majeraha na kushinda kuendelea na mchezo.
Baada ya mchezo huo, kocha Juma Kaseja wa Kagera Sugar, aliwapongeza wachezaji wake kwa kucheza vizuri.
Hata hivyo, Kaseja alisema Simba ilishinda mchezo huo kwa kutumia uzoefu licha ya kuwa pungufu.
Kagera Sugar iliwakilishwa na Said Kipao, David Luhende, Andrew Vicent, Saleh Seif, Hassan Mwaterema, Dikson Mhilu, Daudi Milandu, Fredy Tangalo, Evastus Jali, Mudathir Said na Kasimu Feka.
Simba: Mahamadou Kassali, David Kameta, Libasse Gueye/Bakari Misimu, Yusuph Kagoma, Rushine De Reuck, Morice Abraham, Nikson Kibabage, Ibraheem Jabaar, Ismael Toure, Ibrahim Doumbia na Anicet Oura.



