Na SIMON NYALOBI
BAADHI ya wanasiasa wakongwe nchini, wamesema ushirikiano baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vya ukombozi Kusini mwa Afrika, umezidi kuimarika.
Waliyasema hayo zikiwa ni siku chache baada ya Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Asha-Rose Migiro, kufanya mazungumzo na Katibu wa Chama cha SWAPO cha Namibia, Sophia Shaningwa.
Dk. Migiro na Shaningwa, walikutana na kufanya mazungumzo katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui, Zanzibar mwishoni mwa wiki.
Mazungumzo yao, yalilenga kuimarisha zaidi uhusiano wa kihistoria kati ya CCM na SWAPO, hususan kuongeza ushirikiano na mafunzo ya uongozi kwa vijana, wanawake na taasisi za vyama.
Pia, walijadili umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na kuendeleza mshikamano miongoni mwa vyama vya ukombozi Kusini mwa Afrika.
Akizungumza na gazeti hili jana, Katibu Mstaafu wa NEC ya CCM Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Kanali Mstaafu Ngemela Lubinga, alisema mazungumzo hayo, yamekuwa chachu ya kuimarisha umoja wa vyama hivyo.
Lubinga alisema vyama hivyo ni miongoni mwa vyama sita rafiki vilivyopigania uhuru barani Afrika, ambavyo vimejikita katika kujiimarisha kisiasa, kiitikadi, kiuchumi na kiulinzi.
“Huu ni mwendelezo mzuri wa ushirikiano, ni jambo jema kukutana kwa viongozi hawa, kunaonesha umoja wa vyama hivi bado uko imara,”alisema.
Lubinga alisema vyama hivyo na vingine vinne, vimekuwa katika ushirikiano mkubwa, ambapo ndiyo msingi wa kuanzishwa Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere (MJNLS), iliyopo wilayani Kibaha Mkoa wa Pwani.
“Jitihada za viongozi wa vyama hivyo zimekuwa kubwa, lengo ni kuhakikisha wanachama na mataifa yao wanaendeleza undugu na umoja licha ya kuwepo changamoto mbalimbali,” alisema Kanali Lubinga.
MKUCHIKA
Kwa upande wake, George Mkuchika, alisema CCM inaendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na vyama vingine vya ukombozi kikiwemo SWAPO.
Mkuchika alisema uhusiano mzuri kati ya CCM na vyama hivyo, umekuwa ukirithishwa katika awamu tofauti za uongozi wa vyama na nchi hizo.
“Katika ujana wangu nikiwa Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM mwaka 1979 nilishuhudia uhusiano wa SWAPO na CCM, wakati ule kiongozi wa SWAPO Hayati Sam Nujoma akiendesha mapambano ya kutafuta uhuru wa Namibia akishirikiana na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
“Pia, Rais wa pili wa nchi hiyo, Hifikepunye Pohamba na Rais wa sasa Netumbo Nandi-Ndaitwah, wote hawa wamekuwa wakiimarisha uhusiano wakithamini mchango wa Tanzania, na wanatambua rafiki wa kweli ni yule anayekujali wakati wa dhiki,”alisema.
Mkuchika alisisitiza ushirikiano wa vyama hivyo, ujikite katika masuala ya kiuchumi kama alivyowahi kusema Hayati Nyerere, baada ya nchi hizo kupata uhuru.
Mkuchika ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Urafiki kati ya Tanzania na Msumbiji (TAMOFA), alisisitiza umuhimu wa vyama hivyo kuweka utaratibu wa kubadilishana wanachama na kutembeleana ili kudumisha uhusiano.
“Tujenge utamaduni kila mwaka wanachama wa CCM waende kule na SWAPO wanakuja huku, hii itaimarisha uhusiano wa damu wa vyama hivi,”alisema.
Pia, alishauri kuwepo mikutano ya zamu kila mwaka kwa vyama vyote sita vilivyoshiriki ukombozi wa Bara la Afrika kwa lengo la kudumisha urafiki.
Akizungumzia faida ya mikutano hiyo, alisema itasaidia kubadilishana uzoefu, namna ya kuimarisha uhusiano na kuwaunganisha wanachama pamoja.
MNDOLWA
Naye Mwenyekiti Mstaafu wa Jumuiya ya Wazazi CCM Taifa Dk. Edmund Mndolwa, alisema ameguswa kuona SWAPO inaendelea kutambua mchango wa CCM.
Dk. Mndolwa alisema Tanzania na Namibia zimekuwa na uhusiano wa kindugu kupitia viongozi wa CCM na SWAPO.
Alisema uwepo wa Shule ya Uongozi Mwalimu Nyerere, unaendeleza uhusiano na kuwajengea uwezo viongozi vijana kuongoza vyama hivyo.
Dk. Mndolwa alimpongeza Balozi wa Tanzania nchini Namibia, Ceasar Waitara, kufanya kazi nzuri ya kuwaungania Watanzania na Wanamibia katika ushirikiano wa kindugu na maendeleo.
CCM na SWAPO ni miongoni wa vyama sita vya ukombozi Kusini mwa Afrika, vinavyoshirikiana katika nyanya mbalimbali.
Vyama vingine ni Chama cha African National Congress (ANC) cha Afrika Kusini, ‘Mozambique Liberation Front (FRELIMO) cha Msumbiji, Movement for the Liberation of Angola (MPLA) cha Angola na Zimbabwe African National Union – Patriotic Front (ZANU–PF) cha Zimbabwe.



