ULAANBAATAR, Mongolia
TANZANIA inashiriki Mkutano wa 17 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea Hali ya Jangwa na Ukame (UNCCD COP 17) unaofanyika katika jiji la Ulaanbaatar, Mongolia.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Yussuf Masauni na ujumbe wake, wameshiriki mkutano huo uliofunguliwa na Rais wa Mongolia, Khurelsukh Ukhnaa, Agosti 24, 2026.
Masauni amesema mkutano huo umeweka msisitizo kupitia kaulimbiu yake ya “Ongoa Ardhi, Ongoa Matumaini”, inayohimiza kuongeza uwekezaji katika urejeshaji wa ardhi, ustahimilivu dhidi ya kuenea hali ya jangwa, ukame na usimamizi endelevu wa maeneo ya malisho.
Pia, imetangazwa 2026 ni mwaka wa wafugaji na nyanda za malisho, jambo linalofanya ajenda ya Tanzania kuhusu uhifadhi wa malisho na ustawi wa wafugaji kuwa muhimu zaidi katika mkutano huo.
“Kwa Tanzania, changamoto ya uharibifu wa ardhi inahusishwa na sababu mbalimbali, zikiwemo ukataji na uharibifu misitu, upanuzi wa mashamba kwa kilimo, uchomaji moto usiodhibitiwa, mmomonyoko wa udongo, matumizi yasiyo endelevu ya ardhi na uendelezaji makazi,” amesema Masauni.
Ameongeza: “Ushiriki wa Tanzania katika mkutano huu unatoa fursa ya kupata uzoefu, teknolojia, ushirikiano na rasilimali za kifedha kuimarisha usimamizi endelevu wa malisho, urejeshaji ardhi iliyoharibika, uhifadhi wa misitu, vyanzo vya maji na bioanuwai, pamoja na kuongeza ustahimilivu wa jamii za wakulima na wafugaji katika kupambana na kuenea hali ya jangwa na ukame.
Kwa upande wake, Ofisa Kiungo wa Mkataba huo kutoka Tanzania, Thimoth Mande ameeleza ushirikiano huo unawezesha Tanzania kushughulikia kwa pamoja changamoto za uharibifu wa ardhi, upotevu wa bioanuwai na mabadiliko ya tabianchi, badala ya kuzishughulikia kama changamoto zinazojitegemea.
Amesema ushiriki wa Tanzania siyo wa kuhudhuria mkutano pekee, bali ni fursa ya kuonesha hatua ambazo tayari inachukua katika kupambana na changamoto hiyo, huku ikiomba kuongezewa uwekezaji na teknolojia.
Tanzania inaweza kutumia matokeo ya mkutano huo kuhamasisha rasilimali zaidi kutoka katika mifuko ya fedha za mazingira ambayo ni GEF, IFAD, UNDP, FAO, UNEP, sekta binafsi na mifumo bunifu ya fedha, kuongeza miradi hiyo kutoka kiwango cha maeneo maalumu kwenda maeneo makubwa zaidi.
Naye, Meneja wa Kanda ya Mashariki Kusini, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Aminata Kirama, amebainisha baraza hilo linawajibu wa kupitia maeneo yaliyobainishwa kufanya tafiti.




