Na Cde SHAKA HAMDU SHAKA
AGOSTI 26, 2026, ilikuwa siku ya kihistoria. Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, ilifanya uamuzi mgumu wenye dhamira ya kubeba maslahi mapana ya Taifa.
Maamuzi hayo, yakapata baraka na kukamilika Jumamosi, Agosti 29, 2026 siku ambayo vizazi vijavyo, vitaisoma kwenye vitabu vya kumbukumbu ya nchi yetu.
Lakini kubwa kuliko yote, ni siku iliyojibu swali la vijana wengi: “Je, Taifa letu linatuona?”
Ninaandika haya siyo kama mwanasiasa, bali kama mtoto na kijana wa nchi hii. Ninaandika kutoa shukrani, pongezi na kutoa matumaini kwa vijana na Watanzania kwa ujumla, kufuatia uteuzi wa Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
SHUKRANI KWA RAIS SAMIA
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan.
Watanzania na dunia, tumetambua kazi yako. Tumeona utulivu wako wakati wa dhoruba, tumeona hekima yako katika diplomasia na tumeona upendo wako kwa maskini, mwanamke na mtoto.
Kama ilivyokuwa mwaka 1964 na Mapinduzi ya Zanzibar na Muungano, umeongeza ukurasa mpya kwenye historia. Umeonesha kuwa, wewe ni kiongozi anayesikiliza, anayejifunza na anayebadilika kulingana na mahitaji ya wakati.
Kwa kumteua Makamu wa Rais, Deo Ndejembi, umefanya mambo manne makubwa:
Moja, umeimarisha Umoja: umeonesha kwa vitendo kuwa, Tanzania ni ya wote – wazee, vijana na rika zote.
Mbili, umejenga matumaini; umeonesha kuwa kila kijana ana nafasi ya kulitumikia Taifa lake.
Tatu; umeongeza kasi, umeleta nguvu mpya serikalini ambayo itakuwa chachu ya maendeleo endelevu.
Jambo la nne, umeonesha Dira: umethibitisha kwa vitendo kuwa unafikiria Tanzania ya 2050, siyo 2026 tu.
Rais Samia, wewe ni mama wa taifa na mama wa matumaini ya vijana. Historia itakukumbuka kama kiongozi uliyethubutu. Tunakushukuru.
PONGEZI KWA KAKA YETU
Mheshimiwa Deo Ndejembi, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa niaba ya vijana wa mitaani, vyuo, mashamba na masoko – Hongera sana!
Wewe ni mmoja wetu. Umeota na sisi, umeumia na sisi. Dhamana hii siyo bahati. Ni matokeo ya kazi, nidhamu na uaminifu wako kwa Taifa.
Tunajua mzigo ni mzito. Lakini tuna imani una nguvu ya kuubeba. Jukumu letu ni kukuombea wewe na Mheshimiwa Rais na kuwasaidia pale inapohitajika.
Matumaini ya vijana kwako, yapo katika maeneo matatu:
Moja kuwa sauti yetu, tukumbushe kwenye vikao vya juu kuwa, kuna kijana anataka mtaji, kuna mhitimu anataka ajira.
Mbili, kuwa kioo: Onyesha vijana kuwa nidhamu na kazi ndiyo ufunguo. Kama alivyosema Mheshimiwa Rais: _”Tumeamua kuwamini tena vijana. Nenda kafanye kazi.”_
Tatu kuwa msaada: Msaidie Mheshimiwa. Rais kutimiza ahadi zake kwa kasi.
Mheshimiwa Ndejembi, usiogope wala kujiona mgeni. Taifa zima lipo nyuma yako. Mhe. Rais ni mstari wako wa mbele.
KWANINI NI “TURUFU YA MAENDELEO”
Kihesabu ni rahisi: Dk. Samia + Ndejembi = Turufu ya maendeleo.
Gari kubwa kama Tanzania, haliendi kwa gurudumu moja. Linahitaji turufu yenye nguvu:
Silinda ya Kwanza: Uzoefu na ustawi – Dk. Samia
Uzoefu wa serikalini, mahusiano na dunia, utulivu na moyo wa huruma.
Silinda ya Pili, Nguvu na ubunifu – Mheshimiwa Ndejembi
Uelewa wa lugha ya vijana, kasi ya kufika mashinani, mawazo ya uchumi wa kidijitali na ujasiri wa kuuliza “kwa nini tusifanye tofauti?”
Pamoja, turufu hii italeta matokeo katika:
1. AJIRA: Kuunganisha sera za viwanda + mawazo ya ‘startup’
2. MIRADI MIKUBWA: SGR, Bandari, Nishati – uangalizi wa karibu
3. KILIMO: Teknolojia + Masoko ya Kimataifa
4. ELIMU NA AFYA: Ubunifu wa kidijitali ufike shule na zahanati
5. UMOJA: Kiongozi Mwanamke + Kiongozi Kijana = Tanzania Moja
MWITO KWA TAIFA
Kijana acha kulalamika, tumia fursa. Nchi imefungua mlango.
Kwa Wafanyabiashara; Nchi ni shwari njooni muwekeze serikali ipo.
Viongozi wa Dini: ombeeni na muwe mabalozi wa amani.
Vyombo vya habari: vieneze ukweli na matumaini.
Kila Mtanzania ailinde Tanzania kwa wivu, maendeleo kwa kuwa bila amani ni ndoto kufanikiwa.
Kama vijana tunasema kwa sauti moja: “Mheshimiwa Rais Samia, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Ndejembi, tuko tayari kufanya kazi nanyi.
Mwenyezi Mungu, wape msaada katika kuwatumikia Watanzania, nyoosha hatua zao, wape hekima Luqman, uvumilivu wa Ayubu, na nguvu za Suleiman. Wabariki na uwape afya ili taifa liendelee kusonga mbele.
Tumefunga ukurasa wa matumaini na kufungua wa Kazi, Matumaini na Maendeleo.
Asante Dk. Samia Suluhu Hassan kwa ujasiri,
Hongera Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi kwa dhamana uliyoaminiwa. Wananchi wajibu uko kwetu.
Kazi na Utu Tunasonga Mbele.



