Na MWANDISHI MAALUMU
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amezindua kampeni za ubunge wa Jimbo la Mchinga zilizofanyika katika Kijiji cha Rutamba, mkoani Lindi.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Majaliwa amesema Ilani ya chaguzi ya mwaka 2025/2030 imejielekeza kuendelea kutekeleza miradi ya maendeleo kote nchini ikiwemo katika jimbo hilo.
“Katika kipindi kilichoisha Rais Dk. Samia ameleta hapa miradi mikubwa, ya kati na midogo, anafanya hivi kwa kutambua wananchi wanapaswa kuhudumiwa, hata ilani hii imeonesha maeneo mengine yatakayotekelezwa katika mkoa huu wa Lindi,” amesema.
Amesema wana-Lindi wanapaswa kumchagua mgombea urais kupitia CCM, Dk. Samia Suluhu Hassan aendelee kutekeleza miradi ya gesi, bandari ya uvuvi Kilwa, ujenzi mpya wa barabara ya Dar es Salaam-Lindi, kuboresha uwanja wa ndege wa Lindi, ujenzi wa reli ya kanda ya kusini na kuunganisha mkoa huo katika gridi ya taifa upate umeme wa uhakika.
Amesema Rais Dk. Samia amepeleka mabilioni ya fedha kutekeleza miradi ya maendeleo mkoani Lindi, na Ilani ya chaguzi ya 2025/2030 imeendelea kusheheni miradi ambayo itatekelezwa mkoani humo, hivyo ni sababu kubwa kwa wananchi kumchagua Dk. Samia aendelee kuongoza.
“Ilani ya uchaguzi imeonesha kutaanza kujengwa kwa kiwango cha lami barabara ya Ngongo-Ng’apa, Mandawa hadi Chikundi, barabara hii itakuwa mkombozi kwa wakazi wa maeneo haya na itafungua uchumi kwa wana-Lindi,” ameeleza.
Majaliwa ameongeza katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, jimbo hilo limefanikiwa kuwa na magari ya wagonjwa manne pamoja na ujenzi wa vituo vya afya na zahanati ambazo zimesaidia kuboresha huduma za afya.
“Mheshimiwa Salma Kikwete amejikita katika kuwahudumia wananchi, kwa namna jimbo hili lilivyokaa linahitaj mtu mahiri na mwenye dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi wake, hakika mheshimiwa Salma ameonesha ameweza, mchagueni tena,” alisema.
Kwa upande wake mgombea ubunge wa jimbo hilo, Salma Kikwete alisema katika katika kipindi chake amefanikiwa kushirikiana na wana-Mchinga kutafuta majibu ya changamoto za jimbo hilo.
“Tumepata mafanikio makubwa katika kukabiliana na changamoto zetu, hali ilivyo leo (jana) siyo sawa na tulikotoka, tumepata mafaniko sekta ya afya, nishati, elimu, maji, miundombinu na uwezeshaji wananchi kiuchumi, nikipata ridhaa tena tutafanya makubwa zaidi,” aliahidi.
Alisema kwa kipindi cha miaka mitano amefanikiwa kutekeleza mradi wa maji kutoka Ng’apa ambao utawezesha kuvifikia vijiji vingi vya imbo la Mchinga.
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Kikwete alisema Rais Dk. Samia ameonesha anatosha katika nafasi ya urais, kwa kuwa katika kipindi kifupi amefanya mambo mengi, hivyo anastahili kupewa tena nafasi aendelee kuongoza.
“Alipata urais katika wakati ambao hakutarajia, lakini amefanya kazi nzuri, tutanufaika maradufu, tukimpa nafasi, nimeangalia orodha ya mambo yaliyo katika ilani kwa hakika amejipanga,” alisema.
Akizungumza kwa niaba ya wagombea ubunge mkoa wa Lindi, mgombea ubunge Jimbo la Mtama, Nape Nnauye alisema wananchi wa kusini watamchagua Dk. Samia kutokana na kazi kubwa aliyoifanya kwa mkoa huo ukiwemo utoaji ruzuku ya pembejeo za kilimo.




