Na NJUMAI NGOTA
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimesema kazi kubwa iliyofanywa na serikali chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika kukuza diplomasia ya uchumi, imeongeza idadi ya wawekezaji wakubwa kutoka wastani wa 207 hadi 901.
Hayo yalibainishwa jana katika Viwanja vya Kampala, Gongo la Mboto, Dar es Salaam na Mgombea Mwenza wa Urais wa CCM, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, alipohutubia mamia ya wananchi waliohudhuria mkutano wa kampeni za Chama kuelekea Uchaguzi Mkuu, utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.
Dk. Nchimbi, alisimamisha kwa muda hotuba yake, kupisha adhana, swala la adhuhuri.
Baadaye, aliendelea kwa kusema mafanikio ya wawekezaji, yamechochewa na mazingira rafiki ya biashara, yaliyowekwa na Serikali ya CCM, chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia.
“Vilevile, uwekezaji kazi kubwa imefanywa na Rais Dk. Samia na Serikali ya CCM, katika eneo la diplomasia ya uchumi, miaka minne iliyopita, wawekezaji waliokuja kuwekeza nchini ni 207, wawekezaji wakubwa. Hivi sasa wamefika 901,”alisema.
Dk. Nchimbi, alisema katika miaka mitano iliyopita, leseni mpya zilizotolewa kwa wafanyabiashara nchini ni 137, 318, hivi sasa zimefikia 222,459.
KUHUSU ELIMU
Akizungumzia mafanikio ya kitaifa yaliyopatikana katika miaka minne na nusu ya Rais Dk. Samia, alisema amewezesha ajira mpya kwa walimu wa msingi 38, 394, sekondari 16, 000, ambayo imepunguza uhaba wa walimu na kuinua kiwango cha utoaji elimu nchini.
Alisema amefanya hivyo kwa kutambua kuna walimu wengi ambao wamesomeshwa na serikali na hawajapata ajira.
Akizungumzia sekta ya maji katika Jimbo la Ukonga, Dk. Nchimbi, alisema lengo la serikali ni kuhakikisha kila mwananchi, anapata maji safi na salama, hivi sasa kati ya watu 100 wa Ukonga, 79 wanapata huduma hiyo.
Kwa mujibu wa Balozi Dk. Nchimbi, katika miaka mitano ijayo, wakipewa ridhaa ya kuongoza nchi, CCM imelenga kuhakikisha kila watu 90 kati ya 100, wanakuwa na uhakika wa kupata huduma ya majisafi na salama.
Alisema Ilani ya Uchaguzi ya CCM, imeeleza kwa kina mikakati ya utekelezaji wa miradi ya maji katika maeneo ya Buyuni, Zingiziwa na Msongola na kwamba, serikali itatekeleza mradi mkubwa wa kusambaza maji.
Pia, alisema serikali ijayo ya CCM, imepanga kutekeleza mradi wa upanuzi wa mtandao wa usambazaji maji, utakaonufaisha wakazi wa kata mbalimbali ambazo hazijafikiwa na huduma hiyo, hususan Kata za Buyuni na Nzasa.
Dk. Nchimbi, alisema uzalishaji wa maji wilayani Ilala ukiongezwa kutoka lita milioni 273 hadi kufikia lita milioni 845, hali itakayoboresha kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa huduma hiyo maeneo yote ya jiji.
SEKTA YA MIUNDOMBINU
Katika Sekta ya Miundombinu ya Barabara, Dk. Nchimbi, alieleza kuwa, serikali ijayo ya CCM, imedhamiria kujenga baadhi ya barabara za lami, kupanua na kukamilisha miundombinu ya barabara za mwendokasi hasa Gongo la Mboto na Chanika.
AFYA
Akigusia sekta ya afya, Dk. Nchimbi, alisema serikali ya CCM, imepanga kujenga hospitali mpya ya wilaya eneo la Pugu na vituo vipya vya afya vitatu katika maeneo ambayo bado hayajafikiwa na huduma hiyo, huku kituo cha afya cha Chanika kikitarajiwa kufanyiwa upanuzi mkubwa kukidhi mahitaji ya wakazi wa eneo hilo.
ELIMU
Pia, alisema miaka mitano ijayo, wamekusudia kujenga madarasa 240 katika shule za msingi na mengine 304 kwa shule za sekondari ili kuhakikisha watoto wote, wanapata nafasi ya kusoma katika mazingira bora.
Dk. Nchimbi, alisema katika kuwawezesha vijana kujiajiri, wamekusudia katika maeneo ya mijini, kutoa mafunzo ya ujasiriamali na ufundi.
Katika mkutano huo, Dk. Nchimbi, alimwombea kura kwa wananchi wa jimbo hilo, Mgombea Urais wa CCM, Dk. Samia, wabunge,madiwani na kuwataka wajitokeze kwa wingi Oktoba 29, mwaka huu, kupiga kura na kukipa ushindi Chama Cha Mapinduzi.
JERRY SILAA
Naye, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Ukonga, Jerry Silaa, aliwahakikishia wananchi wa jimbo hilo kuwa, yuko tayari kuendeleza kasi ya maendeleo, akatoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura ifikapo Oktoba 29, mwaka huu.
Pia, alipongeza jitihada kubwa zilizofanywa na Dk. Samia katika kipindi kifupi cha miaka minne na miezi sita.
Alitaja miradi mikubwa ya maendeleo, imetekelezwa katika sekta za barabara, maji, elimu na afya ambayo ni uthibitisho wa dhamira ya kweli ya serikali ya kuleta maendeleo ya watu
CHATANDA
Mratibu wa Uchaguzi wa CCM, Kanda ya Dar es Salaam, Mary Chatanda, alisema uteuzi wa Dk. Samia ni ishara ya heshima kubwa kwa wanawake wa Tanzania.
“Wanawake wa Ukonga na Kivule, wamepokea kwa mikono miwili uamuzi huo wa Chama.
“Wanawake hao, wameahidi kulipa heshima hiyo kwa kumimina kura za kishindo Oktoba 29, mwaka huu,”alisema.
GAVU
Katibu wa NEC, Idara ya Organaizeshi ya CCM, Haji Issa Gavu, aliwaomba wananchi wa jimbo hilo, kuhakikisha wanatoa ridhaa kwa CCM kuendelea kuiongoza nchi kupitia Dk. Samia, wabunge na madiwani.




