Na MUSSA YUSUPH
WAZIRI Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, amesema Mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan ni kiongozi mwenye upeo wa juu na uvumilivu wa kisiasa.
Sumaye, ameyasema hayo wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika Mjini Babati mkoani Manyara, alisema wapinzani wanatamani kianguke jambo ambalo halitowezekana.
“Rais Samia ni mvumilivu. Huyu mama (Dk. Samia) ni mvumilivu sana, ninyi ni mashahidi, wanamsemasema kwa mengi, lakini Mheshimiwa Samia nikwambie, anayepigwa vita siyo Samia, inayopigwa vita ni CCM.
“Wanaokichukia Chama hiki hasa kutoka nje ya nchi, miaka yote wametamani CCM ianguke.
“Kwa hiyo, kinachotafutwa ni CCM kuanguka, sasa wanakuta hii CCM haitikisiki, wanaamua kumshambulia mgombea,” alisema.
Alieleza kuwa, wapinzani wa CCM, wamekuwa wakipuuza nguvu ya chama hicho, badala yake wanamlenga mgombea wake, lakini wananchi watatoa majibu sahihi kupitia sanduku la kura Oktoba 29 mwaka huu.
Kwa upande wake, Mbunge mstaafu Jimbo la Simanjiro, Christoper Ole Sendeka, alitoa wito kwa watia nia, waliokosa uteuzi kugombea ubunge katika mchakato wa kura za maoni, kuvunja makundi.
Alieleza kuwa, wanaCCM wanapaswa kuheshimu maamuzi ya vikao vya uteuzi kwa kuwaunga mkono wagombea walioteuliwa kukiwezesha Chama kupata ushindi.
“Nataka niwaambie viongozi wa Mkoa wa Manyara kama kura zako hazikutosha ameteuliwa mwenzako, mimi nimeonesha mfano kuumunga mkono James Milya na kuwa mratibu wa kampeni zake katika Jimbo la Simanjiro,” alisema.
Naye, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu, Mkoa wa Arusha, Cecilia Paresso, aliwataka wananchi wa Mkoa wa Manyara, kujitokeza kwa wingi siku ya uchaguzi kuwachagua wagombea wa CCM.
Alitoa wito kwa wananchi, kuwaogopa matapeli wa kisiasa wanaopotosha ukweli kuhusu uchaguzi mkuu kwa sababu, nchi inaongozwa kwa kufuata misingi ya kidemokrasia.




