Na REHEMA MAIGALA
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene, amesema ataongoza wizara hiyo kwa kuzingatia ushirikiano, kuheshimu mfumo wa utawala na kuhakikisha miradi na mipango iliyoanzishwa inaendelezwa bila kupoteza rasilimali.
Akizungumza katika makabidhiano ya ofisi hiyo jijini Dodoma, Simbachawene alisema bado ana moyo wa kujitolea na kutumia uzoefu alionao, kujazia mapengo yaliyopo hasa maeneo ambayo aliyawahi kuanzisha kwa misingi thabiti, alipokuwa waziri wa wizara hiyo.
Alisema inasikitisha kuona baadhi ya mambo mazuri yaliyoanzishwa kwa kutumia rasilimali za serikali, yakisimama baada ya wahusika kubadilika.
Alisisitiza kuwa, rasilimali yakiwemo mawazo yaliyowekwa katika maandishi, havipaswi kupotea, hivyo atahakikisha anazitafuta taarifa zote muhimu kuendeleza kazi.
Simbachawene, alisema alikuwa akiandika kwa umakini wakati akikabidhiwa na mtangulizi wake, Innocent Bashungwa, kwa sababu, anatamani kuendelea kujifunza, akibainisha hakuna mtu mwenye haki miliki ya uelewa.
Pia, alisema katika utumishi wa umma, watu husaidiana kufanikisha majukumu, anaamini hata yeye, ataendelea kupata maarifa mapya kila siku, licha ya kuonekana ana uzoefu mkubwa.
Simbachawene aliongeza kuwa yeye ni muumini wa mgawanyo wa majukumu kama ulivyoelezwa katika miundo ya kazi za serikal.
Waziri Simbachawene, alimhakikishia Bashungwa kuwa, atasimamia utendaji kwa kuzingatia utaratibu na nguvu ya mfumo wenyewe.
Pia, alimpongeza Bashungwa kwa kazi kubwa aliyofanya, akisema amefurahishwa na namna alivyoweka mambo katika mpangilio.
Aliahidi kuhakikisha hakuna kazi inayoanza upya bila sababu, bali ataendeleza hatua zilizofikiwa kutimiza malengo.
Kwa upande wake, Bashungwa aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, alisema yuko tayari kushirikiana na Simbachawene wakati wowote akihitajika.




