Na ABDUL DUNIA
KILE kipindi cha msisimko wa soka la Afrika kimewadia, ambapo nchi 24 zitachuana kuwania ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025.
Katika mashindano hayo makubwa zaidi katika soka Afrika, timu zitakazoshiriki ni Morocco, Mali, Zambia na Comoros, Misri, Afrika Kusini, Angola, Zimbabwe, Tanzania, Nigeria, Tunisia na Uganda.
Nyingine ni Senegal, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Benin, Botswana, Algeria, Burkina Faso, Guinea ya Ikweta, Sudan, Ivory Coast, Cameroon, Gabon na Msumbiji.
Msisimko wa michuano hiyo haupo kwa mashabiki pekee bali hadi kwa wachezaji soka na timu zao kutokana na thamani kubwa iliyopo katika mashindano hayo ndani na nje ya uwanja.
Michuano hiyo inatarajiwa kuwakutanisha nyota mbalimbali wakubwa barani Afrika wakiwemo Mohamed Salah anayekipiga Liverpool ya England, Sadio Mane wa Al Nassr ya Saudi Arabia na Sebastien Haller anayecheza Utretch ya Uholanzi.
Pia, yupo Mtanzania Mbwana Samatta anayecheza Le Havre ya Ufaransa, Noah Sadiki wa Sunderland ya England na Youssef En-Nesyri wa Fenerbahce ya Uturuki.
Mbali na nyota hao, pia thamani nyingine ya fainali hizo ni uwepo wa zawadi nono kuanzia kwa bingwa hadi kwa timu itakayoburuta mkia katika hatua ya makundi.
SAFARI YA MABILIONI
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), michuano ya AFCON inatarajiwa kutumia dau la dola za Marekani milioni 32 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 78.3 za Tanzania kwa ajili ya zawadi pekee.
Katika mchanganuo wa fedha hizo, bingwa wa michuano hiyo anatarajiwa kuvuna dola za Marekani milioni saba ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 17.1.
Timu itakayoshika nafasi ya pili itavuna dola za Marekani milioni nne ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 9.7 za Tanzania.
Timu mbili zitakazoishia hatua ya nusu fainali, kila moja itaondoka na dola za Marekani milioni 2.5 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 6.1 za Tanzania.
Timu nne zitakazoishia hatua ya robo fainali zitavuna dola za Marekani milioni 1.3 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 3.1 za Tanzania.
CAF pia imeeleza kwamba, miamba minane itakayoishia hatua ya 16 bora itavuna dola za Marekani 800,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.9 za Tanzania.
Timu zitakazoishia nafasi ya tatu katika kundi, kila moja itaondoka na dola za Marekani 700,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.7 wakati zile zitakazoburuta mkia katika kila kundi zitavuna dola za Marekani 500,000 ambazo ni zaidi ya sh. bilioni 1.2 za Tanzania.
ZILIZOTWAA UBINGWA
Katika michuano hiyo, Misri ndiyo timu iliyotwaa taji hilo mara nyingi zaidi (saba) ikifanya hivyo katika fainali za mwaka 1957, 1959, 1986, 1998, 2006, 2008 na 2010 huku ikifuatiwa na Cameroon iliyobeba mara tano katika miaka ya 1984, 1988, 2000, 2002 na 2017.
Ghana ndiyo inayofuatia ikiwa imetwaa taji hilo mara nne katika miaka ya 1963, 1965, 1978 na 1982 wakati Nigeria ikitwaa mara tatu katika miaka ya 1980, 1994 na 2013 sawa na Ivory Coast iliyobeba katika miaka ya 1992, 2015 na 2023.
Zilizotwaa mara mbili ni Algeria (1990 na 2019) na DRC (1968 na 1974) wakati zilizotwaa mara moja ni Zambia (2012), Tunisia (2004), Sudan (1970), Senegal (2021), Afrika Kusini (1996), Ethiopia (1962), Morocco (1976) na Congo Brazaville (1972).




