GLASGOW, Scotland
PAMBANO la robo fainali ya Kombe la Scotland, ‘dabi’ kati ya Celtic na Rangers limemalizika kwa aibu baada ya mashabiki kuvamia Uwanja wa Ibrox.
Fujo hizo zilisababishwa na mashabiki kutoka pande zote mbili wakivamia uwanja baada ya Celtic kushinda kwa mikwaju ya penalti 4-2 katika pambano lililoshuhudiwa na mashabiki 51,215.
Alikuwa ni Tomas Cvancara aliamsha cheche ndani ya Ibrox alipofunga penalti ya mwisho na kusababisha mashabiki wa Celtic kumiminika uwanjani kusherehekea ushindi kabla ya wafuasi wa Rangers kujibu mapigo kwa kukabiliana na wapinzani wao.
Mashabiki hao walirusha fataki kutoka kwa makundi yote mawili ya wafuasi wa timu hizo huku shabiki wa Rangers alionekana akibebwa na askari baada ya kujaribu kuwavamia wachezaji na mashabiki wa Celtic.
Pia, mashabiki wengine walionekana wakishikilia vipande vya viti vilivyovunjwa vilivyoibiwa katika stendi.
Picha za video zilionyesha chupa zikirushwa kutoka kwa mashabiki wa Gers kuelekea Stendi ya Broomloan, huku viti vilivyovunjika vikirushwa kutoka upande mwingine.
Baada ya tukio hilo, wasimamizi na polisi waliingilia kati kuwatenganisha mashabiki wa timu hizo.
Askari wengi walionekana wamepanda farasi walifika katika eneo la nje ya Stendi ya Broomloan huku kukiwa na fujo za baada ya mchezo. Pia magari ya kutuliza ghasia yalifika kwa kasi katika uwanja huo.
Mkuu wa Polisi , Kate Stephen aliwashutumu mashabiki wote waliohusika katika ghasia hiyo iliyoenea uwanjani hapo.
“Tabia ya wafuasi kadhaa katika mchezo wa robo fainali ya Kombe la Scotland kati ya Rangers na Celtic hapa Ibrox leo(juzi) ilikuwa ya aibu. Ni lazima kulaaniwa na kila mtu anayehusika katika soka na jamii pana.
“Watu kadhaa tayari wamekamatwa, na Polisi Scotland sasa tunafanya kazi na klabu zote mbili na Chama cha Soka cha Scotland kufanya uchunguzi wa kina kufuatia matukio ya uwanjani mwishoni mwa mechi,”alisema.
Stephen aliongeza kuwa maofisa na wasimamizi walikabiliwa na uhasama na vurugu kubwa kwa muda mrefu, huku watu wengi wakiwa wamejizatiti kwa kusababisha madhara.
“ Maafisa na wananchi wamejeruhiwa katika tukio hilo, ningependa kutoa shukrani zangu kwa maofisa na wafanyakazi wote waliopambana kumaliza fujo hizo,”alisema.
Kiongozi huyo wa polisi alisema uc
hunguzi wao, utajumuisha kufuatilia vitendo vya baadhi ya mashabiki walioingia katika stendi iliyopo Barabara ya Broomloan bila tikiti kabla ya mechi kuanza.
“Pia ningemsihi yeyote aliye na habari kuhusu ni nani aliyehusika katika machafuko kabla, wakati au baada ya mechi kuwasiliana na Police Scotland kwa nambari 101,”alisema
Chama Cha Mpira wa Miguu cha Scotland (SFA ) kimethibitisha kuwa uchunguzi utaanzishwa katika tukio hilo la kutisha na limelaani tabia ya wafuasi kuingia uwanja wa Ibrox na kufanya fujo.
Sheria za michuano ya taji hilo, zinaeleza kwamba timu za ugenini zina haki ya kupewa tiketi asilimia 20.
Kocha Mkuu wa timu ya Celtic, Martin O’Neill alisema kitendo cha uvamizi wa ulifunika ushindi wao.
“Ni mchezo mkubwa wa derby na nadhani kulikuwa na shangwe nyingi kwa sisi kushinda. Mashabiki walimwagika na nadhani ni vigumu sana kuzima hilo, sijui.
“Tulipokuwa tukirudi, kulikuwa na hali ya mkanganyiko na kila mtu alijaribu kuingia uwanjani,” alisema.
Kocha Mkuu wa Rangers, Danny Rohl alisema hakuona fujo hizo za uwanja.
“Sikuwepo uwanjani wakati huo, sijaona hadi sasa. Nadhani sote tunajua hali ya hisia baada ya mchezo. Hakuna anayependa kuona hili.
“Ilikuwa hali nzuri kwa dakika 120, na inapaswa kuwa hivi. Mambo mengine hayapaswi kuwa uwanjani au katika sehemu unapochezwa mpira,” alisema.
Rohl alionekana kuhuzunika huku timu yake ikitupwa nje ya michuano hiyo.



