Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa Singida Black Stars umetamba kuwa kikosi chao kipo vizuri kuisambaratisha Simba kesho.
Pia,umewaomba wadau, Mashabiki wa timu hiyo kufika kwa wingi katika Uwanja wa Airtel kuwapa sapoti wachezaji wao washinde.
Timu hizo, zinatarajiwa kucheza Machi 11, mwaka huu katika uwanja huo kuanzia saa 10:15 jioni.
Akizungumza maandalizi ya mchezo huo, Msemaji wa timu hiyo, Hussein Massanza alisema walipoteza mechi dhidi ya Yanga na sasa wamejipanga kuhakikisha wanafanya vizuri.
“Hivi sasa tumerudi katika uwanja wetu, tumejipanga kuhakikisha tunafanya vizuri huu ni mchezo wenye hadhi kubwa.
” Tunafahamu Simba ni timu ambayo imeimarika kwa hiyo tutapambana kwa nguvu zote tuweze kushinda mchezo huo,”alisema.
Massanza alisema mchezo huo, utakuwa na ushindani mkubwa kutokana na uimara wa kikosi cha Simba.
“Tunatarajia kupokea wageni wengi kutoka sehemu mbalimbali lakini tumejipanga kufanya vizuri kwa kuchinja mnyama na kuwapa furaha mashabiki wetu,” alisema.




