Na MWANDISHI WETU
SERIKALI imesema haijawahi na wala haitoanza kulazimisha klabu ifanye mabadiliko bila uamuzi wa wanachama wake.
Uongozi wa Klabu ya Simba, ulifanya Mkutano Mkuu wa Mwaka 2025 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na wajumbe mbalimbali.
Akizungumza katika mkutano huo jijini Dar es Salaam jana, Naibu Waziri Mwinjuma, alisema kwa siku za hivi karibuni kumekuwa na mijadala mingi hasa kuhusu mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji wa klabu ya Simba.
Alisisitiza kuwa serikali haijawahi na wala haitaanza kuilazimisha klabu yoyote nchini kukamilisha mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji bila ya uamuzi wa wanachama wenyewe.
“Serikali haijawahi na wala haitoanza leo kulazimisha klabu yoyote nchini kukamilisha mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji bila ya uamuzi wa wanachama wenyewe,” alisema.
Alisema mchakato wa mabadiliko ya uendeshaji wa klabu ya Simba upo mikononi mwa wanachama wenyewe na serikali hailazimishi.
Hata hivyo, baada ya kauli hiyo, wajumbe walilipuka kwa shangwe ndani ya Ukumbi wa Diamond Jubilee.
“Mchakato huu ni wenu wenyewe ni uamuzi wa wanachama, kama wanachama mtakubaliana kuendelea kuutathmini upya au kubadili mwelekeo, huo utakua uamuzi ambao serikali itauheshimu.
“Jukumu la serikali katika jambo hili ni kuhakikisha kwamba mchakato wote mnaoamua kuutekeleza unazingatia matakwa ya sheria za nchi na kanuni za mchezo huo pendwa nchini.
“Serikali itahakikisha katiba itakayopishwa itakuwa inalinda maslahi ya wanachama, inaheshimu na kulinda maslahi ya wawekezaji waliopo na watakaokuja, inakudhi matakwa ya sheria, kanuni na utaratibu wote unaohusika katika mchakato wa uendeshaji wa klabu za michezo nchini,”.
Alisema jukumu jingine la serikali ni kuhakikisha wanaweka utaratibu utakaoonyesha uwazi, uwajibikaji na utawala bora ndani ya klabu zote.
“Serikali haijatoa na haitoa maelekezo ya kumdhuru mtu yoyote wala kuwaelekeza wanachama jinsi ya kuamua kufanya marekebisho ya jinsi ya kufanya kwa klabu yao.
“Serikali haitoa maelekezo yoyote yatakayoingilia maamuzi ya wanachama kwa mujibu wa sheria, lengo la serikali ni kuhakikisha mjadala wa leo haupotezi mwelekeo kwa mustakabali wa maendeleo ya klabu,” alisema.
Aliwataka wanachama wafanye mjadala kwa utarabu kwa nia ya kuiendeleza klabu ya Simba.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu alisema uongozi huo utazingatia yote kama serikali ilivyoelekeza kwa kufuata utaratibu mzuri na wa haraka.
Alisema wanamshukuru Mwinjuma kutokana na kukubali mwaliko wa mkutano huo ambao upo kwa mujibu wa katiba.
Alisisitiza kuwa awali mkutano huo ulisogezwa mbele kwani uligongana na tarehe ya Uchaguzi Mkuu uliomalizika hivi karibuni.
Alisema baadaye waliomba ridhaa ya vyombo husika kuusogeza mbele kwa ajili ya maslahi mapama ya wanachama.
“Tunakushukuru Naibu Waziri Mwinjuma kwa kukubali wito na kuhudhuria mkutano huu, tunakushkuru.
“Tunaamini utaratibu wa utaendelea kufanyika kwa kuzingatia yote kama serikali ilivyoelekeza kwa kufuata utaratibu mzuri na wa haraka,” alisema.
Aliwataka Wanasimba wasimamie vizuri yale wanayopata ikiwemo kulinda nembo ya klabu kwani imekuwa chachu ya kuleta wadhamini wengi zaidi ndani ya klabu hiyo.
Naye Mhasibu wa Simba, Suleiman Kahumbu alisema wamejipanga kukusanya kiasi cha zaidi ya sh bilioni 29 katika bajeti yake ya mwaka 2025/26.
Alisema fedha hizo zitatokana na vyanzo mbalimbali ikiwemo wadhamini, wawekezaji, viingilio na vingine kuhakikisha klabu inakuwa bora na yenye uwezo wa kujiendesha yenyewe.
“Tumejipanga kukusanya kiasi cha zaidi ya sh bilioni 29 katika bajeti ya mwaka 2025/26, fedha hizo zitatokana na vyanzo mbalimbali ikiwemo wadhamini, wawekezaji, viingilio na vingine kuhakikisha wanafikia malengo,” alisema.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Zubeda Sakuru alisema katika msimu uliopita walipata mafanikio makubwa zaidi ndani ya klabu hiyo.
Alisema msimu uliopita, Simba ilicheza fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAFCC) japokuwa ilimaliza nafasi ya pili katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
Alisema mafanikio hayo yalipatikana kutokana na wanachama na viongozi kuwa kitu kimoja kuhakikisha wanafikia malengo waliyojiwekea.
“Katika msimu uliopita, tulipata mafanikio makubwa kutokana na falsafa yetu ya kusimama imara viongozi, wanachama, mashabiki na taasisi nzima kwa ujumla.
“Katika takwimu sisi tupo nafasi ya tano katika ubora Afrika, tunataka kuhakikisha tunarejea kuwa imara zaidi katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara,” alisema.
Alisisitiza katika Tamasha la 17 la Simba Day mwaka huu, walivunja rekodi ya kuingiza mapato tofauti na ilivyokuwa awali.
Alisema tamasha hilo lilikusanya kiasi cha fedha cha sh. milioni 660 kwa viingilio vya mashabiki pekee huku kwa upande wa udhamini, ilikusanywa takribani sh. milioni 400.




