Na ZIANA BAKARI
JITIHADA kubwa zinazofanywa na serikali kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ni kuhakikisha inawasaidia wasanii kutimiza malengo yao.
Miongoni mwa misaada hiyo ni kutoa mikopo kutoka Mfumo wa Utamaduni na Sanaa Tanzania kwa wasanii, ambapo hupatiwa mikopo kuendeleza kazi zao na kujikimu kimaisha.
Zipo faida mbalimbali zinazotokana na mikopo hiyo, ambayo humsaidia mwigizaji kujiendeleza na kufanya biashara zitakazomsaidia kupata kipato.
Kutokana na serikali kuweka mfumo huo mzuri, wasanii wengi wameibuka na kuonesha vipaji vyao.
Tasnia ya sanaa imepiga hatua kutokana na ushindani uliopo kwa wasanii, kufanya kazi usiku na mchana kwa kiwango kikubwa.
Hali hiyo, imesababisha soko la sanaa hivi sasa, kufanya vizuri na kufuatiliwa na idadi kubwa ya Watanzania, ambao kipindi cha nyuma walikuwa wakiangalia filamu kutoka nje ya nchi.
Pia, ubora wa stori ambazo wanazoziigiza zimekuwa zikiishi katika maisha halisi kwa kuburudisha, kufunza na kutoa onyo.
Baadhi yao wamekuwa wakitumia tasnia hiyo, kuendeleza vipaji vyao na kujipatia kipato cha kuendesha maisha yao.
Miongoni mwa waigizaji ambao wamepata mafanikio makubwa ni Hiza Salum ‘Khizzer’ , ambaye anatamba katika tamthilia ya ‘Jua Kali’ inayoonyeshwa katika kisimbuzi cha Dstv.
Msanii huyo ameoa na kujaaliwa kupata watoto wawili na amekuwa mwigizaji mzuri anayefanya vizuri.
Hivi karibuni, Hiza alihojiwa na gazeti na kufunguka vitu mbalimbali vikiwemo, kazi zake za uigizaji na maisha yake.
Msanii huyo alisema amezaliwa Mkoa wa Tanga na baadaye kuhamia jijini Dar es Salaam.
Alisema katika familia yao yeye ni mtoto wa kwanza kati ya watoto wanne, ambapo mmoja alifariki akiwa bado mdogo.
Hivyo, katika familia yao, wamebaki watatu na kueleza kuwa anaipenda familia yake kwa sababu ya upendo uliopo baina yao.
SAFARI YA KUIGIZA
Msanii huyo alianza kuigiza mwaka 2015 ambapo hadi sasa ana miaka 10 na alipata muda mwingi kujifunza zaidi kuhusu kazi hiyo.
Alijiunga na kundi la Fontana Entertainment ambalo lilikuwa chini ya Mtayarishaji,Neema Ndepanya.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu katika kundi hilo, nilijifunza vitu vingi vya namna tofauti katika kuigiza hadi nilipopata nafasi ya kusimama mbele ya Kamera na kufanya kile ninachokipenda,”alisema.
Msanii huyo alisema haikuwa rahisi siku ya kwanza kuanza kuigiza kutokana na hofu aliyokuwa nayo.
”Nakumbuka nilifanikiwa kushiriki katika filamu ya ‘Kobe la Mchana’ ambayo ilinipa nguvu kubwa ya kuendelea kushiriki filamu zingine tofauti ambazo zilikuwa zikikuza kipaji changu.
“Filamu nyingine ya ‘Mwari wa Uji’ na ‘Kidawa’, ziliendelea kunipa msukumo kwa kuendelea kushiriki filamu zingine ambapo nilifanikiwa kupata mashabiki wengi,” alisema.
Alizitaja baadhi ya tamthilia ambazo amewahi kushiriki kuwa ni ‘Sarafu’ na ‘Jua Kali’ ambayo inaendelea kuonyeshwa katika kisimbuzi cha Dstv.
Msan ii huyo alifafanua kuwa, alifanikiwa kushiriki tamthilia nyingine ya ‘Karma’ iliyokuwa ikionyeshwa katika kisimbuzi cha Dstv.
“Ukishakuwa na kipaji na ukakionesha, basi hata wale watu walikuwa pembeni yako wanakuwa wepesi kukiona na kukupa msaada,” alisema.
Msanii huyo alisema sababu ya pekee iliyomsababisha kuingia katika sanaa ya kuigiza ni kutokana na kipaji alichokuwa nacho.
TAMTHILIA, FILAMU ALIZOZISHIRIKI
Msanii huyo alisema amewahi kushiriki katika filamu na tamthilia nyingi tangu alipoanza kuigiza.
Alizitaja tamthilia hizo ni ‘Sarafu’, ‘Karma’, ‘Mimi’, ‘Yalaiti’, ‘Angel Faces’ na ‘La Familia’.
Alizitaja tamthilia zingine ni ‘Dhohari’, ‘Nice To Meet You’ na ‘Jua Kali’ ambayo bado inaruka katika kisimbuzi cha Dstv.
Akizungumzia filamu alizowahi kushiriki msanii huyo, alizitaja kuwa ni ‘Kobe la Mchana’, ‘Mwari wa Uji’, ‘Mary Mary’, ‘Heaven Sent’ na ‘More Than a Woman’, ‘Merchandizer’.
Akitaja filamu zingine alizoshiriki msanii huyo alisema ni ‘Kidawa’, ‘Niko Sawa’ na zingine.
ANAYOIPENDA
Msanii huyo aliweka wazi kwamba anavutiwa sana na tamthilia ya ‘Jua Kali’ambayo bado inaonyeshwa na uhusika aliopewa.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kuwa miongoni mwa wasanii walioshiriki katika filamu na tamthilia hizo, nafurahi kuona nimekuwa nikiendelea kutoa elimu kwa jamii kwa njia ya kuburudisha na hata kuelimisha.
“Kazi yetu kubwa wasanii ni kuielimisha jamii na kuiburudisha, hii hali inasaidia sehemu kubwa kuwa chachu ya mabadiliko katika jamii kwa sababu, tunavyoelimisha jamii inasaidia kuwajulisha yapi mazuri na mabaya ambayo hayaapaswi kufanywa,”alisema.
CHANGAMOTO
Hata hivyo, msanii huyo alisema kuwa zipo changamoto nyingi wanakutana nazo katika kazi hiyo.
Msanii huyo aliweka wazi kuwa, muda wake wa kupumzika, anapendelea kuwa karibu na familia yake.
“Napenda kufanya mazoezi bila kusahau kucheza mpira na kuogelea,”alisema msanii huyo.
Pia, msanii huyo alisema kuwa, kitu anachopenda kufanyiwa katika maisha yake ni kuheshimiwa.
Mbali na kuigiza, msanii huyo alidokeza kuwa, anajishughulisha na biashara ya ufugaji.
“Namshukuru Mungu ,nafanya biashara ya ufugaji, huko ninapata riziki yangu, kwa ujumla namshukuru Mwenyezi Mungu, napata fedha za kujikimu kimaisha,”alisema.
USHAURI KWA WASANII WENZAKE
Msanii huyo aliwashauri wasanii wenzake, kuendelea kupambana kwa nguvu zote ili kufikia malengo waliyojiwekea.
“Sanaa ni ajira na inalipa, kwa kuwa inasaidia katika sehemu mbalimbali ikiwemo kujikimu kimaisha,”alisema.
Pia, aliishauri jamii kuendelea kuamini kuwa sanaa kuwa ni ajira kama zilivyo ajira zingine.




