Na EMMANUEL MOHAMED
SHIRIKA la Ndege la Tanzania (ATCL), limefanikiwa kuwarejesha nchini Watanzania 236 kutoka maeneo mbalimbali ya Mashariki ya Kati waliokuwa wamekwama, baada mashirika ya ndege kusitisha safari zake kutokana na vita inayoendelea kati ya Marekani, Israel na Iran.
Akizungumza na UHURU jijini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), Gervas Damas, alisema ndege hiyo iliwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 7:46 mchana.
Damas alisema ATCL ilipeleka ndege yake aina ya B787 Dreamliner ambayo iliondoka juzi usiku kwenda Dubai kuwachukua Watanzania waliokwama.
Alisema ndege hiyo ilirejea jana mchana kutokea Dubai na Watanzania hao waliokwama katika jiji hilo, baada ya mashirika ya ndege waliyokuwa wamekata tiketi kusimamisha huduma kutokana na kukosekana hali ya usalama Mashariki ya Kati kufuatia mapigano yanayoendelea.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na ATCL machi 6, mwaka huu, ndege hiyo maalumu ilisafiri kwenda Dubai kuwafuata Watanzania waliokwama na kuwarejesha nchini.
ATCL ilisisitiza ndege hiyo haikuwa ya kibiashara, bali ilikwenda kutoa msaada wa kusafirisha wananchi hao.
Ndege zinazoingia na kutoka viwanja vya ndege vya Tel Aviv, Dubai, Doha na vituo vingine vya kimataifa katika eneo hilo zimesitisha kutoa huduma.
WIZARA YA MAMBO YA NJE
Aidha, taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Afrika Mashariki, iliwaomba watanzania kujisajili kupitia mfumo maalumu wa wizara kwa ufuatiliaji wa karibu na utaratibu wa kupata msaada wa kibalozi endapo ingehitajika kwa mtu yeyote aliyepata changamoto kutokana na mgogoro huo wa Mashariki ya Kati.
Pia, wizara ilielekeza kwa dharura watanzania walipaswa kuwasiliana na balozi za Tanzania zilizo katika miji ya Kuwait, Doha, Abu Dhabi, Ankara na Tel Aviv au Riyadh.
MACHI MOSI, 2026
Machi mosi, mwaka huu, Israel kwa kushirikiana na Marekani, zilianzisha mashambulizi dhidi ya Iran na kusababisha kifo cha kiongozi wa nchi hiyo, Ayatollah Ali Khamenei.
Tangu tarehe hiyo hadi hivi sasa mapigano yamekuwa yakiendelea, hali iliyokwamisha raia wengi wa kigeni kurejea katika nchi zao kufuatia mashirika ya ndege kusitisha huduma za usafiri.




