RABAT, Morocco
KOCHA wa timu ya taifa ya Tunisia, Sami Trabelsi amesema amesema michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2025) imekuwa na upinzani zaidi tofauti na awali.
Tunisia ilitoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Tanzania, katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi uliofanyika Uwanja wa Stade Olympique de Rabat, Morocco.
Kufuatia matokeo hayo, Tunisia imetinga hatua ya 16 bora ya michuano hiyo msimu huu ikiwa na pointi nne nyuma ya Nigeria yenye pointi saba kileleni huku Tanzania ikiingia kama mshindwa bora kwa pointi mbili katika kundi C.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Kocha Trabelsi alisisitiza kwamba michuano ya msimu huu imekuwa na upinzani mkubwa tofauti na ilivyokuwa awali.
Alisema timu zote walizokutana nazo zimejipanga vyema na zina wachezaji wenye uwezo mkubwa, hivyo iliwafanya kutumia mbinu za ziada kupata nafasi ya kusonga mbele.
Alisema anawapongeza wachezaji wake kutokana na kupambana kuhakikisha timu inafanya vizuri na kusonga mbele hatua inayofuata.
“Michuano ya msimu huu imkuwa na upinzani mkubwa, hata kupata pointi ni lazima upambane kwa kiasi kikubwa kwani kila timu imejipanga na ina wachezaji wazuri.
“Ninachoshukuru tumevuka hatua ya makundi, tunakwenda kujipanga vyema kwa mechi zitakazofuata hatua ya 16 bora, ninatambua tutakutana na timu bora zaidi lakini tutatumia uzoefu wetu kufikia malengo,” alisema.




