MANCHESTER, England
UONGOZI wa Klabu ya Manchester United umemtangaza Michael Carrick kuwa kocha wa muda wa kikosi hicho hadi mwishoni mwa msimu huu.
Katika benchi la ufundi hivi sasa, Carrick atasaidiana na beki wa zamani wa England, Steve Holland, Jonathan Woodgate, Jonny Evans na Travis Binnion.
Kiungo huyo wa zamani wa United mwenye umri wa miaka 44, awali alishawahi kuiongoza timu hiyo akiwa kocha wa muda kwa mechi tatu kufuatia aliyekuwa kocha Ole Gunnar Solskjaer kutimuliwa mwaka 2021.
Anatarajiwa kurejea katika Uwanja wa Old Trafford wakati timu yake ikiikaribisha Manchester City katika mchezo wa Ligi Kuu ya England, utakaofanyika keshokutwa.
Manchester United imemtangaza Carrick kuwa kocha wa muda kufuatia Ruben Amorim kutimuliwa kutokana na mwenendo mbovu wa matokeo huku Darren Fletcher akiiongoza kwa muda mechi mbili.
“Ninajisikia faraja kuteuliwa kuwa kocha wa muda na kurejea katika kikosi cha Manchester United rasmi.
“Siamini kama nimechaguliwa mimi, lakini kikubwa ninataka kuhakikisha ninafanya kazi nzuri na kutimiza majukumu yangu ili kuhakikisha ninaondoa presha ya mashabiki iliyopo hivi sasa.
“Ninataka kuonyesha uwezo wa hali ya juu na kuiongoza timu kushinda katika michuano mbalimbali tunayoshiriki msimu huu.
“Ninaamini kila mmoja anatamani kupata burudani kutoka kwa wachezaji wa Manchester United, hilo linawezekana nitarudisha imani iliyopotea kwa muda,” alisema Carrick.
Kabla ya kuteuliwa kuwa kocha wa muda, Carrick alikutana na uongozi wa Manchester United na kukubaliana mambo mbalimbali.
(BBC)




