Na MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameipongeza timu ya taifa ‘Taifa Stars’ kwa kutinga hatua ya 16 bora ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025.
Taifa Stars ilitinga hatua hiyo kwa kanuni ya ‘best looser’ baada ya kumaliza kundi C la michuano hiyo ikiwa nafasi ya tatu kwa alama mbili kufuatia juzi kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Tunisia.
Akiandika kupitia ukurasa wake wa Instagram, Dk. Samia aliimwagia sifa miamba hiyo kwa kuandika historia hiyo kwa mara ya kwanza katika michuano hiyo mikubwa zaidi ya soka Afrika.
“Ninaipongeza timu yetu ya taifa ya mpira wa miguu Taifa Stars kwa kufuzu hatua ya 16 bora ya AFCON kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu.
Heshima hii kubwa kwetu ni matokeo ya maandalizi mazuri na kujituma kwenu katika kila mchezo. Mmeandika historia kubwa kwa Taifa letu na mmeleta furaha kwa Watanzania wote. Hongereni sana,” aliandika Dk. Samia.
Rais pia, aliitakia kila la kheri Taifa Stars katika mchezo wa hatua hiyo dhidi ya Morocco utakaopigwa Jumapili katika Uwanja wa Prince Moulay Abdellah jijini Rabat, Morocco.
Naye Makamu wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, alimuunga mkono Rais Samia kwa kuipongeza Taifa Stars kutinga hatua ya 16 bora.
“Ninaungana na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuipongeza Taifa Stars kwa kufikia mafanikio ya kihistoria ya kufuzu hatua ya 16 bora katika AFCON. Tunawatakia kila la kheri katika michezo inayofuata,” Dk. Nchimbi alitoa pongezi hizo kupitia mtandao wa Instagram.
Katika kundi C, Taifa Stars ilikuwa chini ya kinara Nigeria yenye alama tisa na Tunisia pointi nne na juu ya Uganda iliyoburuta mkia kwa pointi moja.
Tanzania ilianza michuano hiyo kwa kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Nigeria kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Uganda na 1-1 ilipocheza naTunisia.




