Na FRED ALFRED, Dodoma
SERIKALI imekamilisha upembuzi yakinifu wa ujenzi wa reli ya kisasa za mijini katika Jiji la Dar es Salaam na Dodoma.
Hatua hiyo, inalenga kupunguza msongamano wa usafiri wa umma na kuongeza tija katika miji mikuu ya kiutawala na kibiashara nchini.
Kauli hiyo, ilitolewa jijini hapa jana na Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, alipozungumza na waandishi wa habari, kuhusu mafanikio yaliyopatikana ndani ya siku 100 za uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Profesa Mbarawa, alisema Rais Samia, amewezesha kupatikana fedha za msaada kwa usanifu wa kina wa mradi huo, hatua itakayofungua rasmi utekelezaji wake.
“Tumehitimisha upembuzi yakinifu wa ujenzi wa reli ya kisasa kati ya Dar es Salaam na Dodoma. Hatua hii, imefungua fursa ya kupata fedha za msaada za usanifu wa kina, hatimaye utekelezaji wa mradi huu muhimu unaolenga kupunguza msongamano wa usafiri wa umma na kuongeza tija,” alisema Profesa Mbarawa.
BANDARI YA BAGAMOYO
Katika hatua nyingine, Profesa Mbarawa alisema serikali imekamilisha maandalizi ya ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo kwa awamu ya kwanza.
Alisema bandari hiyo ya kimkakati, itapunguza msongamano wa Bandari ya Dar es Salaam na kuiwezesha Tanzania kuwa kitovu cha usafirishaji wa baharini katika ukanda wa Afrika Mashariki.
“Awamu ya kwanza, itahusisha ujenzi wa gati lenye urefu wa kilometa 1.32 kwa ajili ya kuhudumia meli kubwa za kisasa (Mega Max). Bandari hii, itakuwa nguzo muhimu katika kuimarisha uchumi wa nchi,” alisema waziri huyo.
Vilevile, alisema wizara imekamilisha mchakato wa kuanza upanuzi mkubwa wa Bandari ya Dar es Salaam, unaolenga ujenzi wa magati 10 na matanki 15 ya mafuta.
Alisema ujenzi wa magati mawili ya awali yenye urefu wa meta 500 unatarajiwa kuanza Juni mwaka huu, huku ujenzi wa matanki ukiendelea kutekelezwa.
“Uboreshaji huu utaongeza uwezo wa Bandari ya Dar es Salaam kuhudumia shehena hadi tani milioni 50 kwa mwaka, kutoka tani milioni 32 za sasa,” alisema Profesa Mbarawa.
SEKTA YA ANGA
Akizungumzia sekta ya anga, Profesa Mbarawa alisema serikali imeendelea kupanua na kuboresha huduma za usafiri wa anga kupitia Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL).
Alisema katika kipindi hicho, ATCL imeongeza vituo vipya vya safari katika miji ya Victoria Falls nchini Zimbabwe, Cape Town (Afrika Kusini) na Accra (Ghana) na kufikisha jumla ya vituo 32.
Alifafanua kati ya vituo hivyo, 15 vya ndani ya nchi, 14 ndani ya bara la Afrika na vitatu vya kimataifa nje ya Afrika.
“Ufunguzi wa vituo vipya, umeimarisha muunganiko wa safari na kuongeza ufanisi pamoja na urahisi kwa wananchi kupata huduma za usafiri wa anga,” alisema Profesa Mbarawa.




