Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, ameiagiza Wizara ya Nishati, kuongeza kasi ya kupanua mtandao wa usambazaji gesi asilia, kukidhi mahitaji ya taifa.
Amesema kwa kufanya hivyo, kutawawezesha wananchi kupata nafuu ya gharama katika uendeshaji wa vyombo vya moto na matumizi mengine ya nishati pamoja na serikali kupunguza matumizi ya fedha za kigeni, kuagiza mafuta.
Dk. Mwigulu, amesema hayo jijini Dar es Salaam, alipozindua Kituo Mama cha Gesi Asilia Iliyosindikwa (CNG) cha Puma Energies, kilichopo Salasala. Ujenzi wa kituo hicho, umegharimu takribani shilingi bilioni 13.
“Wizara ya Nishati, endeleeni kuongeza kasi ya utafutaji wa gesi asilia, iwe nishati ya kawaida ya maisha ya kila siku ya Mtanzania.
“Watanzania jitokezeni kwa wingi kutumia fursa ya uwepo wa gesi asilia iliyoshindiliwa,”amesema.
Waziri Mkuu, amesema uzinduzi wa mradi huo, unaakisi utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Nishati na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Vilevile, inaendana na mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, wa kuhakikisha rasilimali za nishati, hususan gesi asilia, zinatumika kama kichocheo cha maendeleo ya viwanda, usafiri na uzalishaji wa umeme,”amesema.
Amesema mradi huo, unaashiria hatua muhimu katika utekelezaji wa mkakati wa Taifa wa kuhamia katika matumizi ya nishati safi, salama, nafuu na uhakika kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
“Kwa kufanya haya, Puma Energies, mmeunga mkono kwa vitendo jitihada za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, za kuijenga Tanzania inayotumia nishati safi,”amesema.
Dk. Mwigulu, amesema serikali itaendelea kuchukua hatua za kuboresha mazingira ya uwekezaji, ikiwemo kuhakikisha uwepo wa sera thabiti, mifumo rafiki ya udhibiti, uwazi katika utoaji wa uamuzi na ushirikiano wa karibu kati ya taasisi za serikali na sekta binafsi.
“Serikali inathamini mchango wa sekta binafsi katika kutekeleza miradi ya maendeleo na utoaji wa huduma kwa umma.
“Serikali imeendelea kushirikiana na sekta binafsi katika ujenzi wa vituo vya gesi asilia iliyoshindiliwa,”amesema.
Amesema katika kipindi cha siku 100 za Rais Dk. Samia madarakani, serikali imewezesha upatikanaji wa majiko banifu 13,575 yenye ruzuku ya asilimia 85 na mitungi ya LPG 28,653 ya kilo sita yenye ruzuku ya asilimia 50.
“Vilevile, serikali imewezesha taasisi 89 zinazolisha watu zaidi ya 100 kwa siku kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia na hivyo kufikia taasisi 1,136.”
Naye, Naibu Waziri Wizara ya Nishati, Salome Makamba, amesema miongoni mwa maeneo yanayokua kwa kasi katika matumizi ya gesi asilia ni sekta ya usafirishaji kupitia matumizi ya Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (CNG), ambapo hivi sasa zaidi ya vyombo vya moto 15,000 nchini vinatumia CNG.
Amesema kuwa, hadi kufikia Januari, mwaka huu, vituo vya kujazia CNG vilikuwa 11 ambapo tisa vipo Jiji la Dar es Salaam, kimoja kipo mkoani Pwani na kingine Mtwara.
“Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi tumeweka mpango wa kuongeza idadi ya vituo kufikia 20 ifikapo Juni, 2026 hususan katika Mikoa ya Morogoro na Dodoma, kuhakikisha upatikanaji wa huduma za CNG katika miji mikubwa na katika barabara kuu za usafirishaji,”amesema.




