Na VICTOR MKUMBO
KATIKA kuendelea maandalizi ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027), Kamati ya Kitaifa ya mashindano hayo, imeanza kuweka mikakati madhubuti ya ulinzi na usalama michezoni.
Hayo yalielezwa katika kikao cha kamati hiyo kilipokutana na Mkuu wa Kitengo cha Usalama wa Michezo kutoka Umoja wa Mataifa (UN), Valeroo de Divitiis, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Michezo, Boniface Tamba alisisitiza umuhimu wa kuweka mikakati madhubuti ya ulinzi na usalama itakayohakikisha mashindano ya AFCON 2027 yanafanyika katika mazingira salama.
Alisisitiza michuano hiyo ambayo itashirikisha mataifa mbalimbali ya Afrika, inatakiwa kufanyika katika hali ya utulivu na inayokidhi viwango vya kimataifa.
Alibainisha kuwa Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi waandaji, ina wajibu wa kuhakikisha miundombinu ya viwanja, mifumo ya udhibiti wa umati, na usimamizi wa matukio makubwa ya michezo vinaimarishwa kwa kuzingatia miongozo ya kimataifa.
Alisema kikao hicho kililenga kuimarisha uratibu kati ya taasisi za usalama na michezo, kufanya tathmini ya vihatarishi (risk assessment) na kuweka mifumo thabiti ya usimamizi wa usalama itakayohakikisha Tanzania inatimiza wajibu wake kama mmoja wa waandaji wa mashindano hayo makubwa barani Afrika.
“Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi waandaji, ina wajibu wa kuhakikisha miundombinu ya viwanja, mifumo ya udhibiti wa umati na usimamizi wa matukio makubwa ya michezo vinaimarishwa kwa kuzingatia miongozo ya kimataifa,” alisema.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya AFCON 2027, Leodegar Tenga alisema dhamira ya serikali na wadau wa michezo ni kuhakikisha mashindano ya AFCON 2027 yanafanyika kwa mafanikio makubwa.
Alifafanua mafanikio hayo ni nje ya ubora wa kiufundi wa michezo, bali kwa viwango vya juu vya ulinzi na usalama.
Msimu ujao wa fainali za michuano ya AFCON 2027, zinatarajiwa kufanyikia katika nchi za Tanzania, Kenya na Uganda.





