Na MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa zawadi ya sh. milioni 50 kwa timu ya Taifa ya Wanawake ya Tanzania ‘Twiga Stars’ ikiwa ni sehemu ya hamasa kwa kufuzu kucheza fainali za Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON 2026), zitakazofanyikia nchini Morocco.
Twiga Stars ilifuzu michuano hiyo baada ya kuichapa Ethiopia kwa mabao 3-0, ikishinda 2-0 nyumbani na kuitandika 1-0 ugenini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, alisema Rais Dk. Samia ametoa fedha hizo ikiwa ni hamasa kwa Twiga Stars.
Alisema wamepewa fedha hizo kuhakikisha wanajipanga vyema kwenda kushiriki katika fainali za WAFCON 2026 zitakazofanyika Machi, mwakani nchini Morocco.
Alisisitiza Rais Dk. Samia anawapongeza Twiga Stars kwa kufuzu kucheza fainali hizo msimu ujao.
“Rais Dk. Samia ametoa kiasi cha sh. milioni 50 kwa Twiga Stars kutokana na kufuzu kucheza fainali za WAFCON 2026.
“Amewapongeza na ametuelekeza kuhakikisha timu haishuki kiwango na itaendelea kufanya vizuri zaidi katika michuano mbalimbali itakayoshiriki,” alisema Msigwa.
Alisema serikali itaendelea kutoa sapoti kwa timu hiyo na kuendeleza mpango wake wa kutumia michezo kimkakati ikiwemo kuvutia watalii na wachezaji kupata ajira nje ya nchi.




