Na ELIZABETH JOHN
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali imejipanga kikamilifu kulinda nchi, mipaka, raia na mali zao wakati wote.
Aliyasema hayo, alipokuwa akizungumza na Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC).
Alisema ana taarifa baadhi ya watu, wamepanga kuingia barabarani kuandamana Desemba 9, mwaka huu au katika Sikukuu ya Krismasi Desemba 25, kwa lengo la kufanya vurugu, hivyo amewataka waliopanga mpango huo, kusitisha kwa kuwa Serikali ipo imara.
Kwa mujibu wa Rais Samia, waliopanga kuingia barabarani, wana ajenda binafsi ya kutaka kuchochea vurugu na kuhatarisha amani ya nchi, hivyo Serikali haitakubali hali hiyo itokee.
“Lingine linapangwa, mola hatosimama nao litapeperuka, nilimsikia mmoja kati ya waandamanaji wa nje, anasema Desemba 09, mwaka huu, wahairishe maandamano hadi Desemba 25 siku ya Krismasi, kwa sababu sasa hivi wamejipanga, nataka kuwaambia wakati wowote wakija tumejipanga,” alisema.
Rais Dk. Samia, alisema kabla ya vurugu zilizotokea Oktoba 29 mwaka huu, Tanzania ilikuwa moja ya visiwa vya amani duniani kwa kutambulishwa kwa amani na umoja.
Alisema kila siku zinavyozidi kwenda sifa hiyo imeendelea kuporomoka kutokana na kukereka kwa wenye wivu wa amani ya Tanzania.
Alisema vurugu si desturi wala utamaduni wa Tanzania, kila aliyepoteza maisha ni Mtanzania na hakuna mwenye sababu ya mambo hayo kuendelea.
“Kila aliyeumia au kupoteza maisha ni Mtanzania mwenzetu, mwenye haki sawa na mwingine, hakuna mtu aliye juu ya mwingine, haki ya kuishi na haki ya kuwa huru ni tunu zetu wote Watanzania.
“Kwa hiyo, hakuna sababu ya Watanzania kuumizana na kunyimana uhuru,” alisema Dk. Samia.
Alisema inatia uchungu, kuona walioratibu fujo wakitaka Watanzania wenzao kuwa kafara kwa malengo yao ya kisiasa yenye ubinafsi.
Pia, Rais Samia, alisema kilichotokea Oktoba 29, mwaka huu, hayakuwa maandamano, ni vurugu zilizoandaliwa kwa madhumuni maalumu, hivyo nguvu iliyotumika kuyadhibiti, inaendana na tukio husika.
“Takwimu zinatolewa sasa hivi, kuna majengo kadhaa ya Serikali yameunguzwa, kuna miradi kadhaa iliyojengwa kwa maslahi ya wananchi imeunguzwa, vituo vya mafuta, biashara binafsi za watu, magari ya serikali, vituo vya Polisi vingi tu vimeunguzwa, sasa hayo ni maandamano au vurugu?
“Maandamano tuliyoyazoea na kuyakubali ndani ya katiba ni yale watu wameudhika na kitu, tunaomba tuandamane tueleze tutatoka pointi moja hadi Mnazi Mmoja au popote pengine na mabango yanaeleza maudhui yetu na polisi wanawasindikiza vizuri hadi wanapofika.
“Haya ya kuunguza miradi ya Serikali, vituo vya polisi na kwenye kituo cha Polisi unakwenda kufanya nini? ni kwenda kuvamia na wapate silaha, madhumuni ya kuwa na silaha mkononi ni nini? Haya hayakuwa maandamano, zilikuwa vurugu zilizoandaliwa kwa madhumuni maalumu.
“Tunaapa kuilinda mipaka ya nchi hii, raia na mali zao, katika hali hiyo, nguvu inayotumika inaendana na tukio lililopo, tunapoambiwa tulitumia nguvu kubwa sana kwenye tukio lile… nguvu ndogo ilikuwa ni ipi? Ilikuwa tuwaangalie waandamanaji waliojiandaa kufanya mapinduzi mpaka wafanikiwe? Hapo patakuwa na dola kweli? Dola haipo hivyo.
“Na siyo Tanzania tu, hata mataifa mengine, watu wakiandamana wanaweka nguvu kubwa, sasa wanapokuja kutulaumu mlitumia nguvu kubwa wao walitaka nini?, tujiulize, je hawa ndiyo wafadhali wa kile kilichofanyika? “Walitaka tuangalie hadi wafanikiwe walichowatuma? Hapana! tuliapa kulinda nchi hii na mipaka yake, usalama wa raia na mali zao kwa hiyo, kama wanavyofanya wao na sisi tutafanya vilevile kuilinda nchi yetu,” alisema Rais Dk. Samia.
Alisema vijana waliofanya vurugu, waliingizwa katika maandamano bila kuelewa sababu wala madai yao, wengi wao waliimbishwa wimbo wasioujua.
Rais Dk. Samia, alisema baadhi ya vijana wamekuwa wakimezeshwa taarifa zisizo sahihi kuhusu hali ya maisha nchini, hali inayosababisha wapotoshwe kirahisi na kutumiwa na makundi yenye maslahi ya kisiasa. Alisema vurugu zilichochewa na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani, ambao walikosa uzalendo na waliopanga kwa makusudi kusababisha machafuko mbali na kupewa fursa za kufanya siasa kwa uhuru na kuheshimiwa na Serikali.
Rais Samia, alisema baadhi ya viongozi wa upinzani, wanapandikiza misimamo ya uchochezi kwa wananchi wakati ndani ya vyama vyao kuna migogoro ya ndani, makundi na kuvunjika kwa umoja vimewafanya kushindwa kuona mbele.




