Na WAANDISHI WETU
AJENDA ya umoja imetawala mahubiri ya Pasaka, baada ya Maaskofu kusema ni msingi mzuri wa kujenga ustawi wa taifa na wananchi wake.
Wito huo ulitolewa na viongozi wa dini kwa nyakati tofauti nchini, katika mahubiri ya Ibada ya Sikukuu ya Pasaka.
MALASUSA
Akizungumza katika mahubiri hayo, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Malasusa, alitoa wito kwa Watanzania kudumisha amani na upendo.
Dk. Malasusa alisema hayo alipotoa ujumbe wa Sikukuu ya Pasaka, katika ibada iliyofanyika Kanisa la Azania Front, jijini Dar es Salaam.
“Anapofufuka Yesu itukumbushe na sisi kufufua mazuri ambayo Mungu ameyaweka katika familia, maisha yetu, taifa letu ikiwemo kutetea umoja wa kitaifa,” alisema Dk. Malasusa.
Dk. Maslasusa alisema umoja, upendo ni sifa na tunu ya taifa letu, hivyo aliwasisitiza Watanzania kushikamana, kupendana na kuishi maisha yenye furaha.
“Tuendelee kushikamana, tupendane, tusameheane na tushikane pale tunapoona mwenzetu ameanguka. Tukaribishane katika kanisa wakati wote,”aliongeza.
ASKOFU SOSTHENES
Kwa upande wake Askofu wa Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Dar es Salaam, Jackson Sosthenes, alitoa wito kwa waumini wa dini ya Kikristo na wananchi kudumisha amani, upendo na kuvumiliana.
Askofu Sosthenes, alisema jamii inapaswa kuishi kwa amani na upendo siku zote kwa kuwa hujengwa katika misingi ya mafundisho ya dini inayohimiza watu kuheshimiana, kusaidiana na kutobaguana.
“Niwasihi sana waumini wanaposheherekea Sikukuu hii ya Pasaka kutanguliza mbele masuala ya amani, kusimamia mafundisho ya dini yanayotolewa na kumuenzi Yesu Kristo muda wote.
“Tuendelee kuishi kwa upendo, kuheshimiana na kusaidiana kuepuka vitendo vinavyoweza kuvuruga utulivu uliopo nchini kwetu, niwaombe kushikamana na kuimarisha maadili mema yanayojenga taifa lenye amani na umoja,” alisema Askofu Sosthenes.
Aidha, alisema kila muumini anapaswa kupokea na kuomba msamaha kwa kila aliyemkosea, kwa kuwa Pasaka ni ishara ya kurejea utukufu wa Mungu uliopotea, ukiwakumbusha waumini kuhusu neema, msamaha na upendo wa muumba kwa binadamu.
PAROKO WIGIRA
Paroko wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Padri Denis Wigira, alisema waumini wanapaswa kuitumia sikukuu hiyo kama fursa ya kutafakari upya maisha ya kiroho.
Padri Wigira alisema waumini wana wajibu wa kuimarisha uhusiano wao na Mungu kwa njia ya sala, toba na matendo mema.
“Leo tunasherehekea Pasaka kufufuka kwa Yesu Kristo, niwasihi sana waumini kusherehekea sikukuu hii kwa amani, furaha na upendo.
“Tunaposherehekea sikukuu hii tunasherehekea ukombozi wetu, tunapaswa kuishi kwa kuhurumiana na kuombana msamaha baina yetu,”alisema.
Alisisitiza kuwa, jamii inayodumisha amani huchochea umoja na mshikamano miongoni mwa wanajamii, hatua inayochangia ustawi na maendeleo.
Kuhusu umuhimu wa kudumisha amani, Padri Wigira aliwashauri Watanzania kuendelea kutambua umuhimu wake kuwa ni tunu ya taifa inayopaswa kulindwa na kuthaminiwa na kila mmoja.
“Tunapaswa kufahamu Kristo ni mfalme wa amani, amani ya kweli ina sadaka ndani yake na amani ya kweli ni katika kuishi maisha ya haki, tudumishe maisha ya kweli na tutendeane haki,”alisema.
ASKOFU CHOLONGANI
Akizungumza katika mahubiri ya Pasaka, Askofu Mkuu wa Kanisa Kuu la Roho Mtakatifu, Dayosisi ya Central Tanganyika, Dk. Dickson Cholongani, aliiomba serikali kuongeza nguvu ya kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
Cholongani alisema pamoja na mafanikio yaliyopatikana; baadhi ya wananchi wanakutana na changamoto zinazopunguza ustawi na furaha yao zikiwemo rushwa, ukiritimba na kunyimwa haki katika baadhi ya taasisi za umma.
“Tunashukuru mwaka jana mishahara iliongezwa, lakini bado kuna changamoto katika baadhi ya ofisi za umma. Kuna ukiritimba, kunyimwa haki na rushwa,”alisema Dk. Cholongani.
Aidha, Dk. Cholongani alisema: “Naipongeza serikali kwa juhudi za kusimamia ulinzi wa amani, umoja na mshikamano nchini.”
Pia, aliitaka jamii kushiriki kikamilifu kujenga taifa lenye maadili mema, akibainisha kipindi cha Pasaka ni fursa ya kuleta mabadiliko chanya, kurejesha matumaini na kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi.
PAROKO MSALABA
Kwa upande wake Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Paulo wa Msalaba, Kanisa Kuu la Jimbo Katoliki la Dodoma, Chrisant Mganga, alisema baadhi ya watu wamezama katika uovu kwa kutosikiliza mapenzi ya Mungu.
“Mungu anaruhusu tuchapike na maradhi halafu hapo tunamkumbuka, kwamba yeye ndiyo kila kitu, hivyo tunapoomba tuwe tunamshukuru maana yeye ndiyo anatuwezesha, tusimkumbuke katika shida tuu,” alisema.
ASKOFU KINYAIYA
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dodoma, Beautus Kinyaiya, alikemea baadhi ya watu wenye tabia ya kuweka taarifa za vifo vya watu mitandaoni bila idhini.
Kinyaiya alisema kitendo hicho siyo tu kinakiuka maadili, pia kinapuuza utaratibu rasmi wa utoaji taarifa ndani ya taasisi na familia husika.
“Kilichopo unaweza kukuta Padri au Sista wa kanisani amefariki, badala ya kupewa taarifa kiongozi wa kanisa, unazikuta zimerushwa mitandaoni na nyimbo zimeshaandikwa, mpaka mhusika anashangaa,” alisema.
Aliwashauri waumini wa dini ya Kikristo kuachana na mambo ya kibinadamu yasiyo na tija, akisisitiza kuwa Yesu Kristo tayari alishayashinda kupitia kifo na ufufuko wake.
Katika hatua nyingine, Askofu Kinyaiya alitoa wito kwa familia kuhakikisha watoto wanapata malezi bora bila kuathiriwa na migogoro ya wazazi au walezi wao.
“Tujue mtoto umleavyo ndivyo atakavyokuwa, tuwape malezi, elimu na imani nzuri wawe tegemeo zuri katika taifa letu, tuwarithishe mila njema na tuwasaidie katika makuzi yao kujenga taifa letu,” alisema.
ASKOFU MUSHENDWA
Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Magharibi, Jackson Mushendwa, alitoa wito kwa waumini wa dini ya Kikristo duniani kote kuomba na kusali kukomesha vita inayoendelea maeneo mbalimbali duniani.
Mushendwa alisema hayo katika Ibada ya Pasaka iliyofanyika Kanisa la KKKT, Dayosisi ya Magharibi Usharika wa Kigoma.
Alisema hivi sasa dunia imekuwa siyo sehemu salama ya kuishi, kwa kuwa vita imesababisha madhira na maumivu makubwa kwa binadamu.
Kwa mujibu wa Askofu Mushendwa, kufufuka Yesu Kristo kuwe mwanzo wa kuzaliwa kwa mwanzo mpya wa kuiombea dunia na Tanzania kuondokana na madhira hayo.
Askofu Mushendwa alisema risasi, mabomu na kila aina ya silaha havitamaliza vita duniani, bali mazungumzo na kukaa meza moja kati ya pande zinazopingana kuondoa tofauti zao.
Mushendwa alisema, hakuna dini wala siasa yenye haki ya kutoa uhai wa watoto wasio na hatia au kufanyiwa vitendo vya ukatili.
Imeandikwa na Rehema Mohamed, Hawa Ngadala, Ziana Bakari, Selina Mathew na Fadhili Abdallah




