Na MWANDISHI WETU
SERIKALI kupitia Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Bohari ya Dawa (MSD) wameanza hatua mpya ya kimkakati ya kuimarisha usalama wa kifedha katika mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya nchini.
Kufanikisha hatua hiyo, kimefanyika kikao kazi kilichokutanisha wizara ya afya, MSD na wateja wao 45 kujadili namna bora ya kuondoa na kudhibiti madeni ya taasisi zinazohudumiwa na MSD.
Akifungua kikao hicho, katika Ukumbi wa Mkemia Mkuu jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Emmanuel Tayari, alisema serikali imekusudia kuona wateja wote wa MSD wanashiriki kujenga mfumo endelevu wa kifedha utakaoihakikishia bohari hiyo uwezo wa kuendelea kutoa huduma bila kuyumba.
“Ni muhimu sasa wadau wote tukajadili kwa kina na kuja na mpango madhubuti, endelevu na wa pamoja wa kuondoa madeni ya MSD na kuzuia hali hii kujirudia. Pia ni muhimu wadau kukaa na kuzungumzia ubinifu zaidi katika kuboresha upatikanaji wa bidhaa za afya ili kuwa na uhakika wa afya bora kwa Watanzania.
“Kila taasisi inapaswa kuona wajibu wake katika kuimarisha afya ya kifedha ya MSD kwa kulipa au kupunguza madeni yaliyopo,” alisema Tayari.
Mfamasia Mkuu wa Serikali, Daudi Msasi akizungumza katika kikao hicho, alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa mfumo madhubuti wa usimamizi na udhibiti wa madeni katika hospital zote zinazohudumiwa na MSD kuzuia kujirudia kwa changamoto ya ongezeko la madeni.
“Ni wakati sasa wa kuweka ukomo wa deni kwa taasisi zinazopokea huduma za MSD pamoja na kuwa na mpango endelevu wa malipo. Aidha, MSD inapaswa kusimamia kikamilifu sheria na utaratibu kuzuia mrundikano wa mikopo usiohimilika kwa wateja wake,” alisema.
Aliongeza kuwa, changamoto hiyo inapokuwa kubwa huathiri uwezo wa MSD kununua moja kwa moja kutoka viwandani, pamoja na kupanga akiba ya kimkakati ya bidhaa muhimu za afya, jambo ambalo linaweza kuhatarisha uthabiti wa huduma za afya nchini, hususan wakati wa dharura na milipuko ya magonjwa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai, alisema ongezeko la madeni ya taasisi mbalimbali limeendelea kuathiri uwezo wa bohari hiyo kutekeleza majukumu yake ya msingi, hususani ununuzi ya bidhaa za afya na ulipaji wa washitiri.
“MSD ina jukumu kubwa la kuhakikisha upatikanaji endelevu wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya kutolea huduma nchini kote.
“Hata hivyo, ongezeko la madeni kutoka kwa baadhi ya hospitali linaathiri mtiririko wa fedha na hivyo kupunguza uwezo wetu wa kufanya ununuzi kwa wakati, kulipa wazabuni na kuendeleza huduma muhimu za ugavi wa bidhaa za afya,” alisema.
Akichangia mjadala, Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Profesa Abel Makubi, alisema changamoto ya madeni haiwezi kutatuliwa kwa kuangalia MSD pekee, bali inahitaji tathmini pana ya mfumo mzima wa kifedha wa sekta ya afya nchini.
Baadhi ya wateja wa MSD walieleza kuwa, licha ya dhamira ya taasisi nyingi kutaka kulipa madeni hayo, hali ya kifedha inayotokana na gharama kubwa za uendeshaji wa huduma za afya imekuwa changamoto kubwa kwa baadhi ya hospitali na taasisi.




