Na MWANDISHI WETU
SERIKALI imevunja ukimya kuhusu mjadala na kura iliyopigwa na Bunge la Ulaya kuhusu Programu ya Ubia kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya (EU) ya mwaka 2026, yenye thamani ya Euro milioni 156, ikisisitiza taarifa zinazosambazwa kuhusu kusimamishwa kwa fedha hizo si sahihi, kwani uhusiano kati ya pande hizo mbili unaendelea vizuri kupitia majadiliano.
Taarifa iliyotolewa jana na Kitengo cha Mawasiliano kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ilieleza kuwa, serikali ilifuatilia mjadala na upigaji kura uliofanyika katika Bunge la Ulaya Juni 18, mwaka huu, kuhusu Programu ya Ubia kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya kwa mwaka 2026 yenye Jumla ya Euro milioni 156.
HOJA ZA UHUSIANO
“Serikali imebaini kuwa, baada ya upigaji kura huo, kumekuwa na taarifa mbalimbali katika baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zinazotoa tafsiri isiyo sahihi kuhusu maana ya kura hiyo. Kutokana na hali hiyo, Serikali inapenda kutoa ufafanuzi ufuatao:
“Kwanza, kura iliyopigwa katika Bunge la Ulaya si uamuzi wa mwisho wa Umoja wa Ulaya kuhusu Programu ya Ubia na Tanzania kwa mwaka 2026. Kura hiyo ni sehemu ya mchakato wa ndani wa taasisi za Umoja wa Ulaya likiwemo Bunge hilo, limetoa maoni na mapendekezo yake kwa mamlaka nyingine zinazohusika na uamuzi wa mwisho,” ilieleza.
Taarifa ilifafanua, kinyume na baadhi ya taarifa zinazosambazwa, mapendekezo yaliyotolewa na Bunge la Ulaya siyo kusimamishwa kwa fedha za programu za ubia zinazotekelezwa au kutarajiwa kutekelezwa nchini, hivyo kilichopendekezwa na Bunge hilo ni kufanyiwa mapitio programu hiyo na kuwasilishwa tena.
“Aidha, kwa mujibu wa taratibu zilizopo mapitio yoyote ya programu ya ubia hufanyika kwa mashauriano na makubaliano ya pande zote mbili na hatimaye kuridhiwa kupitia Mkataba wa Pamoja wa Fedha (Joint Financial Agreement) kati ya Serikali na Umoja wa Ulaya. Hivyo, maamuzi hayo si ya upande mmoja na hayatakuwa hivyo,” ilieleza.
Ilieleza kuwa, ni muhimu kwa umma kufahamu katika jumla ya Euro milioni 156 zinazozungumziwa, kiasi kilichokuwa kimepangwa kuelekezwa moja kwa moja serikalini kupitia mifumo rasmi ya serikali ni Euro milioni 17 pekee.
Wizara iliongeza, pia kiasi kilichobaki cha takribani Euro milioni 139 kilipangwa tangu awali kutekelezwa kupitia taasisi teule za Umoja wa Ulaya, taasisi za nchi wanachama wa umoja huo na asasi za kiraia, hivyo tangu awali, sehemu kubwa ya fedha za programu hiyo haikuwa imepangwa kuingia moja kwa moja katika mifumo ya Serikali.
Sehemu ya taarifa hiyo ilisisitiza, baadhi ya hoja zilizomo katika azimio lililopitishwa haziakisi kikamilifu ukweli na uhalisia wa hali halisi ya Tanzania na hatua zinazoendelea kuchukuliwa na serikali baada ya matukio ya Oktoba, mwaka 2025.
Vilevile, serikali ilitoa ufafanuzi wa kina kuhusu hatua hizo kwa Bunge la Ulaya na kwa wabunge wote wa Bunge hilo, kabla ya upigaji wa kura, hivyo kusikitishwa kwamba pamoja na ukweli huo kujulishwa, hoja zilizo katika azimio hilo hazijazingatia ukweli huo.
“Serikali inapenda kuwahakikishia wananchi kuwa uhusiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Ulaya ni imara, ni ya kirafiki na ya kimkakati na yanaendelea kuimarika katika maeneo mbalimbali yenye manufaa kwa pande zote mbili.
“Aidha, tuna mifumo rasmi ya kushauriana na kuwasiliana kwenye masuala yote yanayogusa uhusiano huo kila kunapokuwa na hitaji hilo,” ilieleza taarifa hiyo.




