Na HANIFA RAMADHANI, Zanzibar
UMOJA wa viongozi wa vyama 12 vya siasa Zanzibar, umewataka viongozi, wanachama na wananchi, kuunga mkono na kulinda maridhiano ya pamoja kwa vitendo.
Pia, umekemea kauli za chuki, uchochezi, ubaguzi na vitendo vyovyote vitakavyohatarisha amani na mshikamano wa Zanzibar.
Vyama vinavyounda umoja huo ni Chama Makini, UPDP, Ada Tadea, UMD, DP, CCK, TLP, NLD, SAU, NCCR-Mageuzi, UDP na NRA.
Kauli hiyo ilitolewa Mjini Unguja na katibu wa umoja huo ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Makini, Ameir Hassan Ameir.
Alikuwa akitoa tamko kwa niaba ya vyama 12 vya siasa visiwani Zanzibar, kuhusu maridhiano ya kisiasa yaliyofanyika kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT- Wazalendo.
“Tunatoa rai kwa taasisi zote za umma, viongozi wa serikali, vyama vya siasa na wadau, kuhakikisha tamko la maridhiano, linaendelea kuishi katika matendo, uamuzi na mwenendo wetu wa kila siku,” alisema.
Alisema katika mazungumzo ya maridhiano, siyo kila jambo lililojadiliwa linapaswa kuwekwa hadharani, isipokuwa kuna hekima kubwa ya kuheshimu usiri wake.
Alisema kufanya kinyume chake, kutadhoofisha imani, kuvuruga utekelezaji wa makubaliano na kuhatarisha mafanikio ya mchakato mzima.
“Tunasisitiza kuwa, ikiwa kuna haja ya kutoa taarifa kwa umma kuhusu utekelezaji wa makubaliano au hatua zilizofikiwa ni vyema taarifa hizo zitolewe kwa utaratibu uliokubaliwa na pande husika na pale inapowezekana zitolewe kwa pamoja,” alisema.
Alisema utaratibu huo, hujenga uaminifu, huondoa tafsiri zinazokinzana na huimarisha mshikamano kati ya wahusika.
Ameir, aliwahisi viongozi wa kisiasa na wanaharakati, kujiepusha na matumizi ya majukwaa ya kisiasa au mitandao ya kijamii kutoa tafsiri binafsi, siri za vikao, kauli zinazoleta taharuki au maneno yanayoibua migawanyiko.
Alisema wanatambua maridhiano hayo, yanakusudia kuendeleza mazungumzo ya kisiasa kama njia bora ya kutatua tofauti, kuondoa migawanyiko isiyo ya lazima, kuimarisha demokrasia na kujenga imani miongoni mwa vyama vya siasa.
Kwa mujibu wa Ameir, mafanikio ya maridhiano hayatategemea kutiwa saini kwa makubaliano, isipokuwa namna yatakavyoheshimiwa, kulindwa na kutekelezwa kwa uaminifu na busara.
Aliwataka viongozi wa vyama vya siasa, wanaharakati, wafuasi wa vyama na wadau wa kisiasa, kuheshimu kikamilifu, madhumuni na masharti ya makubaliano yaliyofikiwa.
“Maridhiano ya kweli hujengwa juu ya misingi ya kuaminiana, kuheshimiana na kuwajibika kwa kauli na matendo,” alisema.
Aliwapongeza viongozi wa vyama vya CCM na ACT -Wazalendo kwa uamuzi wao wa kuweka mbele maslahi ya taifa, amani na ustwi wa wananchi.
Julai 9, mwaka huu, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT Wazalendo, walitia saini tamko la pamoja la mariadhiano ya kisiasa.
Akizungumza baada ya kutiwa saini kwa tamko hilo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, alisema ni hatua ya kihistoria itakayodumisha umoja, mshikamano na amani.
Dk. Mwinyi, alisema tamko hilo la maridhiano, litaweka msingi imara wa maendeleo ya kiuchumi na kijamii Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.
Alisema tamko hilo, linaonesha dhamira ya kweli ya vyama hivyo, kuendelea kushirikiana kutafuta suluhisho la kudumu na endelevu la changamoto za kisiasa zinazoikabili Zanzibar.
Dk. Mwinyi alisema hatua hiyo ni mwanzo wa utekelezaji wa matakwa ya katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, yanayowezesha uundwaji wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kwa mujibu wa masharti ya kikatiba.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa ACT -Wazalendo Taifa, Othman Masoud Othman, alisema mafanikio ya mchakato wa maridhiano ya kisiasa Zanzibar, yanahitaji ushirikiano wa wananchi wote huku akisisitiza umuhimu wa kuweka pembeni maslahi ya vyama na watu binafsi kwa ustawi wa Zanzibar.




